Waziri Mkuu mpya wa Ethiopia auzuru mji uliokuwa kitovu cha maandamano dhidi ya serikali
Waziri Mkuu mpya wa Ethiopia jana Jumatano aliahidi kuzipatia ufumbuzi changamoto zinazoukabili mkoa anakotoka wa Oromo; ambao umekuwa kitovu cha machafuko makubwa yaliyotishia uhai wa muungano wa chama tawala nchini Ethiopia.
Abiy Ahmed aliapishwa kuwa Waziri Mkuu wa Ethiopia tarehe Pili mwezi huu baada ya mtangulizi wake Haimemariam Desalegn kulazimika kujiuzulu mwezi Februari mwaka huu. Abiy aliye na umri wa miaka 42 ambaye ni afisa wa zamani wa jeshi anakabiliwa na changamoto za kuyapatia ufumbuzi na kumaliza hasira na malalamiko ya vijana wa kabila lake la Oromo ambalo ni kabila kubwa zaidi nchini Ethiopia. Watu wa kabila hilo wanalalamika kwamba wamekuwa wakibaguliwa kisiasa na kiuchumi huko Ethiopia.

Mara baada ya kuwasili katika eneo hilo jana Jumatano, Abiy Ahmed alilakiwa na maelfu ya watu wa mji wa Ambo mkoani Oromiya. Mji huo umekuwa kitovu cha maandamano dhidi ya serikali tangu mwaka 2015 ambapo mamia ya watu wanatajwa kuuawa kati ya mwaka 2005 na 2017.
Akiwa ziarani katika mkoa wa Oromiya, Waziri Mkuu wa Ethiopia ameahidi kutatua masaibu na changamoto zote zinazoutatiza mkoa huo.