Imamu akatwa shingo na kuuawa katika hujuma msikitini Afrika Kusini
Magaidi wakufurishaji wameuvamia msikiti karibu na mji wa Durban Afrika Kusini na kumua shahidi Imamu kwa kumkata shingo na kuwajeruhi waumini wengine kadhaa.
Taarifa zinasema Alhamisi alasiri magaidi hao waliokuwa na silaha waliuvamia msikiti wa Waislamu wa madhehebu ya Shia katika mji mdogo wa Verulam nje ya Durban na kuwashambulia kwa visu waumini akiwemo Imamu wa Msikiti wa Imam Hussein AS ambapo walimuua kwa kumchinja shingo lake. Waumini wengine waliodungwa visu wamejeurhiwa vibaya. Magaidi hao waliokuwa na visu na bunduki walitoroka kwa gari aina ya Hyundai na polisi wamesema wameanzisha oparesheni ya kuwasaka.
Kaimu Kamishna wa Polisi katika Jimbo la KwaZulu-Natal Meja Bheki Langa amesema magaidi hao pia waliteketeza moto sehemu moja ya msikiti kabla ya kutoroka. Amesema Afrika Kusini haiwezi kustahamili jinai kama hiyo na kwamba maafisa wa usalama wanachunguza tukio hilo.
Baadhi ya duru zinadokeza kuwa waliotekeleza hujuma hiyo ya kikatili ni raia wa Misri lakini polisi bado hawajaweza kuthibitisha hilo.
Jumuiya ya Maulamaa Afrika Kusini imetoa taarifa na kulaani mauaji hayo na kusema yanaleng akuibua taharuki, na hali ya kutokuaminiana katika jami.
Waislamu ni karibu asilimia 1.9 ya watu wote milioni 55 nchini Afrika Kusini na ni nadra misikiti kuhujumiwa. Lakini katika wiki za hivi karibuni kumeshuhudiwa ongezeko la chuki dhidi ya Waislamu wa madhehebu ya Shia katika mitandao ya kijamii jambo ambalo limeibua wasiwasi mkubwa miongoni mwa Waislamu nchini humo.