Zuma azidi kusakamwa, kesi dhidi yake yawasilishwa mahakamani
https://parstoday.ir/sw/news/africa-i4777-zuma_azidi_kusakamwa_kesi_dhidi_yake_yawasilishwa_mahakamani
Kiongozi wa jamii ya Khoisan nchini Afika Kusini amewasilisha kesi ya jinai dhidi ya Rais Jacob Zuma wa nchi hiyo.
(last modified 2023-11-27T08:44:11+00:00 )
Apr 10, 2016 03:31 UTC
  • Zuma azidi kusakamwa, kesi dhidi yake yawasilishwa mahakamani

Kiongozi wa jamii ya Khoisan nchini Afika Kusini amewasilisha kesi ya jinai dhidi ya Rais Jacob Zuma wa nchi hiyo.

Zuma kwa sasa anakabiliwa na mashinikizo ya kila upande kumtaka ajiuzulu baada ya Mahakama ya Katiba kutoa uamuzi kuwa rais huyo wa Afrika Kusini alikiuka katiba na kuhujumu mkondo wa sheria.

Stanley Petersen ambaye anaongoza vuguvugu jipya la kisiasa la ‘Mapinduzi ya Khoisan’ amesema wafuasi wa jamii hiyo wameshindwa kuvumilia ubadhirifu wa fedha za umma unaofanywa na serikali ya Rais Zuma. Amesema maendeleo ya msingi yamekosa kufika katika kila pembe ya nchi kutokana na kufumbiwa macho ufisadi unaofanywa waziwazi na maafisa na wanasiasa wa chama tawala ANC na wapambe wa Rais Zuma.

Haya yanajiri siku chache baada ya Zuma kunusurika kura ya kutokuwa na imani naye bungeni. Mbali na wanaharakati, wapinzani wa serikali ya Afrika Kusini wamemtaka Rais Zuma ajiuzulu kwa madai ya kuruhusu ufisadi serikalini.

Itakumbukwa kuwa, hivi karibuni Jaji Mkuu wa Afrika Kusini, Mogoeng Mogoeng aliipa Wizara ya Fedha ya nchi hiyo siku 60 kuamua ni kiasi gani cha fedha Zuma anapaswa kuzirejesha katika hazina ya taifa, kati ya zaidi ya dola milioni 16 za Marekani, zilizotumika kuifanyia ukarabati nyumba yake binafsi katika eneo la KwaZulu Natal.