Watunisia wapinga kuwepo kijeshi Marekani nchini kwao
Hatua ya vyama mbalimbali nchini Tunisia kupinga uwepo wa wanajeshi wa Marekani nchini humo imeipelekea washington iachane na msimamo wake katika uwanja huo.
Vyama mbalimbali vya Tunisia vimelalamikia uamuzi wa Kamandi ya Jeshi la Marekani barani Afrika (Africom) wa kutaka kutuma wanajeshi wa Marekani huko Tunisia kwa ajili ya kusimamia matukio ya huko Libya. Kufuatia uamuzi huo wa Africom, chama cha Leba cha Tunisia kimetaja kuwepo wanajeshi wa Marekani nchini humo kuwa ni kitendo hatari kwa mamlaka ya kitaifa ya Tunisia na kwamba kitaitumbukiza Tunisia katika mapigano ya ndani huko Libya.
Chama hicho kimesema kuwa Africom inaingilia mgogoro wa ndani wa Libya ili kupora utajiri wa maliasili ya nchi hiyo yakiwemo mafuta na gesi.
Chama cha Leba cha nchini Tunisia aidha kimekosoa na kutaja kimya cha viongozi wa nchi hiyo kwa tangazo la Africom kuwa ni ishara ya kukubali serikali ya Tunis uwepo wa wanajeshi wa Marekani huko Tunisia.
Chama hicho kimevitolea wito pia vyama vyote vya kisiasa na taasisi za kiraia nchini kusimama imara dhidi ya hatua hiyo ya Africom na kutoruhusu nchi yao kugeuzwa kuwa kituo cha kijeshi cha Marekani ili kuingilia masuala ya ndani ya Libya na kukariri senario ya Syria huko Libya.