Jeshi la la Algeria laua na kukamata magaidi 12
Wizara ya Ulinzi ya Algeria imetangaza habari ya kuuawa watu wanane wanaoaminika kuwa wanachama wa makundi ya kigaidi kusini mwa mji mkuu wa nchi hiyo Algiers.
Taarifa ya wizara hiyo imesema kuwa, magaidi hao wameuawa katika operesheni ya leo Jumapili katika eneo la Rouakeche, kusini mwa mji mkuu wa nchi hiyo ya kaskazini mwa Afrika. Habari zaidi zinasema kuwa, wanachama wengine wanne wa magenge hayo ya kigaidi wamekamatwa katika operesheni hiyo huku wanajeshi wa nchi hiyo wakinasa shehena ya silaha zilizokuwa zikitumiwa na magaidi hao. Hata hivyo taarifa ya Wizara ya Ulinzi ya Algeria haijaweka wazi jina au majina ya magenge ya kigaidi ya watu hao waliouawa na kumakatwa katika operesheni ya leo.
Mwishoni mwa mwezi uliopita wa Mei, watu sita wanaoaminika kuwa wanachama wa makundi ya kigaidi waliuawa na jeshi la Algeria katika mkoa Bouira, kusini mashariki mwa nchi hiyo.
Katika miezi ya hivi karibuni jeshi la Algeria limeimarisha msako dhidi ya wanachama wa makundi ya kigaidi kama vile al-Qaeda katika eneo la Maghrib AQIM, Boko Haram la nchini Nigeria na lile la Daesh la nchini Libya, ambayo yanafahamika kwa kutenda jinai dhidi ya binaadamu.