Jun 17, 2024 10:47 UTC
  • Watu 21 wafariki dunia na kujeruhiwa baada ya basi la kanisa kuteketea kwa moto Zimbabwe

Takriban Wakristo saba wa Kanisa la Anglikana Dayosisi ya Manicaland waliokuwa wanatoka katika ibada ya kanisa la Bernard Mzeki mjini Marondera wameteketea kwa moja katika ajali mbaya iliyotokea eneo la Gandanzara wilayani Makoni baada ya basi walilokuwa wakisafiria kuwaka moto ghafla.

Basi hilo ambalo ni mali ya shirika la usafiri la Passion Link, liliteketea kwa moto usiku wa kuamkia leo Jumatatu karibu na Kituo cha Biashara cha Gandanzara, kilichoko umbali wa takriban kilomita 44 kutoka mji wa Rusape wa mashariki mwa Zimbabwe.

Jeshi la Polisi wa la Zimbabwe (ZRP) limethibitisha kutokea ajali hiyo mbaya kupitia ukurasa wake rasmi wa mtandao ya kijamii wa X.

Ijapokuwa polisi hawakuweza kutoa maoni yao mara moja, lakini askari wa usalama wa barabarani kutoka Rusape waliofika eneo la tukio wamesema kuwa takriban watu saba wanahofiwa kuteketea kwa moto na sura zao haziwezi kutambulika kutokana na kuungua vibaya.

Baadhi ya abiria wamenusurika kwenye moto huo mkali sana ambao umepelekea basi zima kuteketea vibaya.

Baadhi ya vyombo vya habari vimesema kuwa, takriban watu 14 wamejeruhiwa baadhi yao wako katika hali mbaya na wamewahishwa kwenye hospitali kuu ya mji wa Rusape kwa matibabu.

Waziri wa Uchukuzi na Maendeleo ya Miundombinu wa Zimbabwe, Felix Mhona na Waziri wa Nchi anayeshughulikia masuala ya Mkoa wa Manicaland pamoja na Wakili wa Ugatuzi, Misheck Mugadza wametembelea eneo la ajali hiyo.

Kila mwaka Wakristo wa Kiangalikana hukusanyika pamoja kwenye kaburi la Bernard Mizeki huko Marondera kutoka kona zote za Zimbabwe bali pia kutoka maeneo mengine ya kusini mwa Afrika na kwingineko.

Tags