Apr 16, 2024 10:49 UTC
  • Amir-Abdollahian: Iran haitoruhusu Israel kuhatarisha usalama wa ukanda huu

Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran amesema kuwa, Jamhuri ya Kiislamu ya Iran inaamini kwamba usalama na utulivu wa nchi za eneo hili zima ni muhimu sana kwake, bali ni sawa kabisa na usalama wake yenyewe na haitoruhusu utawala wa Kizayuni kuhatarisha usalama wa eneo hili kwa chokochoko zake.

Kwa mujibu wa shirika la habari la IRNA, Hossein Amir-Abdollahian amesema hayo katika mazungumzo ya simu na Waziri mwezake wa Mambo ya Nje wa Oman, Sayyid Badr Al-Busaidi na kumueleza msimamo wa Tehran kuhusu matukio ya eneo hili hususan shambulizi la kijeshi lililofanywa na Iran dhidi ya utawala wa Kizayuni baada ya Israel kushambulia ubalozi mdogo wa Iran mjini Damascus, Syria.

Kwa upande wake, Waziri wa Mambo ya Nje wa Oman amelaani jinai za utawala wa Kizayuni hususan dhidi ya wananchi madhlumu wa Palestina na kutilia mkazo wajibu wa kuweko mashauriano na uratibu wa pamoja wa nchi za ukanda huu hasa katika kipindi hiki nyeti na tete mno baada ya Iran kuutia adabu utawala wa Kizayuni.

Mawaziri wa Mambo ya Nje wa Iran na China

 

Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran amefanya mazungumzo pia na Waziri wa Mambo ya Nje wa China, Wang Yi, na kumueleza jinsi Jamhuri ya Kiislamu ilivyochukua hatua za kidiplomasia kwanza kufuatilia jinai ya Israel ya kushambulia ubalozi wa Iran mjini Damascus na ilipoona imekwamishwa na madola ya Magharibi ya Marekani, Uingereza na Ufaransa, ikalazimika kuushambulia kijeshi utawala wa Kizayuni ili kuutia adabu usirudie tena. 

Waziri wa Mambo ya Nje wa China amesema kwenye mazungumzo hayo kuwa nchi yake inapinga kushambuliwa maeneo ya kidiplomasia na kwamba shambulio la Israel kwenye ubalozi wa Iran mjini Damascus lilikanyaga sheria na misingi ya kimataifa. 

Tags