Jun 28, 2024 11:30 UTC
  • Khatibu wa Sala ya Ijumaa ya Tehran awataka wananchi wachague mgombea bora

Imam wa Sala ya Ijumaa iliyosaliwa leo hapa Tehran amesema kuwa, shahid Ebrahim Raisi, Rais wa Iran aliyefariki dunia kwa ajili ya helikopta, alikuwa hajui kuchoka na ni kigezo kizuri cha kuchagua mgombea bora wa urais anayefanana naye ili ashike nafasi yake.

Kwa mujibu wa shirika la habari la Mehr, Sheikh Kazem Siddiqi ameongeza kuwa, shahid Raisi kama alivyokuwa Shahid Beheshti, walikuwa wakifanya kazi usiku na mchana bila ya kuchoka katika kulitumikia taifa na wananchi, hivyo kama tunataka kuchagua mtu anayefaa zaidi kushika nafasi ya rais ajaye wa Iran, basi lazima tuzingatie vigezo hivyo viwili na tuhakikishe kuwa ni mtu muumini, aliyeshikana na dini, anayeona mbali, mwenye mtazamo mpana na aliye bora zaidi kuliko wengine.

Amesema, imani anayopaswa kuwa nayo Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran lazima iwe zaidi ya watu wa kawaida kwani yeye ni mtu muhimu sana katika nchi, hivyo imani yake kwa misingi ya Mapinduzi ya Kiislamu inapaswa iwe kubwa zaidi kuliko watu wengine wa kawaida.

Khatibu wa Sala ya Ijumaa ya Tehran vile vile amewataka wananchi wapiga kura wawe makini sana katika uchaguzi wao na kuwakumbusha kitu muhimu akiwaambia: Imam Khomeini MA alikuwa na imani na vitu kadhaa, kumwamini Mwenyezi Mungu, kuamini njia aliyoichagua na kuamini uungaji mkono wa wananchi. Amesema, Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran anapaswa kuwa rais wa wananchi asiyependa makuu, kama alivyokuwa shahid Ebrahim Raisi.