Jun 29, 2024 12:56 UTC
  • Uchaguzi wa rais wa Iran waingia duru ya pili; Pezeshkian kuchuana na Jalili

Matokeo rasmi na ya mwisho ya duru ya 14 ya uchaguzi wa rais wa kabla ya wakati wa Iran yanaonesha kuwa zoezi hilo litaingia katika duru ya pili.

Duru hiyo ya pili ya uchaguzi iliyopangwa kufanyika Julai 5, itawachuanisha aliyekuwa Waziri wa Afya na mbunge wa sasa, Masoud Pezeshkian na mkuu wa zamani wa timu ya mazungumzo ya nyuklia, Saeed Jalili. 

Mohsen Eslami, Msemaji wa Makao Makuu wa Uchaguzi ya Iran amesema baada ya kuhesabiwa kura zote zilizopigwa (24,535,185) kwenye uchaguzi huo wa Ijumaa ya jana Juni 28, Pezeshkian ameibuka kidede kwa kupata kura 10,415,991 huku Jalili akiambulia kura 9,473,298.

Kwa mujibu wa matokeo hayo yaliyotangazwa na tume hiyo ya uchaguzi ambayo ipo chini ya Wizara ya Mambo ya Ndani  ya Iran, wagombea wengine wawili, Spika wa Bunge, Mohammad Baqer Qalibaf na waziri wa zamani wa mambo ya ndani, Mostafa Pourmohammadi, wameshika nafasi ya tatu na nne, kwa kura 3,383,340 na 206,397 kwa utaratibu huo.

Uchaguzi wa Rais Iran

Tayari Qalibaf ambaye amewahi pia kuwa Meya wa jiji la Tehran amewaasa wafuasi wake wampigie kura Jalili katika duru ya pili ya uchaguzi huo itakayofanyika Ijumaa ijayo. Wairani wasiopungua milioni 61 walitimiza masharti ya kupiga kura.

Wagombea hao wanne walichuana kuwania kiti cha Urais kilichobakia wazi baada ya kufariki dunia aliyekuwa Rais wa Iran, Shahidi Ebrahim Raisi katika ajali ya helikopta, tarehe 19 Mei mwaka huu.

Wagombea wengine wawili wa Urais, Amirhossein Ghazizadeh Hashemi na Alireza Zakani walijiondoa kwenye kinyang'aniyiro hicho kabla ya uchaguzi wenyewe kufanyika jana Ijumaa.

Tags