Jun 29, 2024 08:12 UTC
  • Ayatullah Ali Khamenei
    Ayatullah Ali Khamenei

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amewataja Walinzi wa Haram kuwa ni waokozi wa Iran na eneo la Magharibi mwa Asia.

Ayatullah Ali Khamenei amesema katika kikao na wajumbe wa Kongamano la Kimataifa la Mashahidi wa Muqawama na Walinzi wa Haram kuwa ni tukio la kustaajabisha na muhimu na moja ya madhihirisho ya mtazamo wa kiulimwengu wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran. Amesisitiza kuwa: Kuwepo vijana wa mataifa mbalimbali katika sura ya Walinzi wa Haram kulionyesha kuwa Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran yana uwezo wa kuibua upya hamasa ya kipindi cha mwanzoni mwa mapinduzi hayo baada ya kupita zaidi ya miongo minne.

Ayatullah Khamenei ameongeza kuwa: Kuwepo vijana ambao hawakumuona Imam Khomeini (RA) na zama za Vita vya Kujitetea Kuakatifu katika harakati ya wapiganaji ya Walinzi wa Haram Tukufu kumeonyesha nguvu ya ajabu ya Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran katika kuunda upya msukumo na hamasa ya kidini na kimapinduzi ya miongo minne iliyopita.

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amekutaja kushiriki wapiganaji wa harakati ya Walinzi wa Harami katika nchi ambazo adui alikuwa amepanga njama hatari sana dhidi yao, kuwa ni mojawapo ya madhihirisho ya mtazamo wa kiulimwengu wa Mapinduzi ya Kiislamu ya Iiran.

Amesema: Katika mipango yake, adui alikuwa na lengo la kuangamiza utawala wa Kiislamu nchini Iran kwa kulikalia kwa mabavu eneo la Magharibi mwa Asia na wakati huo huo kuiwekea Iran mashinikizo ya kiuchumi, kisiasa na ya kiitikadi na kimadhehebu; lakini kundi la vijana wenye imani, chini ya uongozi wa Jamhuri ya Kiislamu, limezima na kubatilisha mpango huu wenye gharama kubwa wa kibeberu.

Ameashiria ukatili mkubwa wa kundi la Daesh (ISIS) na makundi yanayofungamana nalo ambayo yaliundwa kwa msaada wa silaha na propaganda za Marekani na nchi za Magharibi kwa ujumla na kusema kuwa: Lengo la kundi hilo lilikuwa kuvuruga amani ya eneo la Magharibi mwa Asia, hasa Iran, lakini Walinzi wa Haram walizima hatari hiyo kubwa.