Jun 29, 2024 08:11 UTC
  • Zoezi la kuhesabu kura za uchaguzi wa rais wa Iran linaendelea, Jalili na Pezeshkiyan wanakabana koo

Zoezi la kuhesabu kura za uchaguzi wa rais wa Iran uliofanyika jana kote nchini bado linaendelea huku matokeo ya awali yaliyotangazwa na Tume ya Uchaguzi yakiashiria ushindani mkali kati ya wagombea wawili, Saeed Jalili na Masoud Pezeshkian.

Baada ya kuhesabiwa zaidi ya kura milioni 19, inaonekana kwamba kuna mchuano mkali kati ya waziri wa zamani wa afya na mbunge wa sasa, Masoud Pezeshkian na mkuu wa zamani wa timu ya mazungumzo ya nyuklia, Saeed Jalili.

Wagombea wengine wawili, Spika wa Bunge Mohammad Baqer Qalibaf na waziri wa zamani wa mambo ya ndani, Mostafa Pourmohammadi - wametimuliwa kivumbi na kubakia nyuma kwa sasa. 

Matokeo ya kura zaidi ya milioni 19 zilizohesabiwa hadi tunaingia mitamboni yalionyesha kuwa, Pezeshkian alikuwa amepata kura 8,302,577, Jalili kura milioni 7,189,756, Qalibaf kura 2,676,512 na
Pourmohammadi kura 158,314.

Wairani wasiopungua milioni 61 walitimiza masharti ya kupiga kura.

Wagombea wanne wanachuana kuwania kiti cha Urais kilichobakia wazi baada ya kufariki dunia aliyekuwa Rais wa Iran Shahidi Ebrahim Raisi katika ajali ya helikopta, tarehe 19 Mei mwaka huu.