Apr 22, 2016 04:37 UTC
  • Brigedia Jenerali Pordastan: Iran kuadhibu vikali wavamizi

Kamanda wa Jeshi la Nchi Kavu la Iran amesema chokochoko zozote dhidi ya Jamhuri ya Kiislamu zitapata jibu kali na kwamba vikosi vya ardhini vya Iran vitawaadhibu vikali wavamizi.

Brigedia Jenerali Ahmad Reza Pourdastan amesema hayo katika mkutano na wambata wa kijeshi wa nchi za kigeni hapa mjini Tehran na kuongeza kuwa, vikosi ya ardhini vya Iran vilivyo na silaha za kisasa zilizotengenezewa hapa nchini, viko imara na tayari kujibu uchokozi wa wavamizi na maadui wa taifa hili.

Hata hivyo, Kamanda wa Jeshi la Nchi Kavu la Iran amesisitiza kuwa, uwezo wa kijeshi wa Jamhuri ya Kiislamu ni kwa ajili ya kujihami na kuzima hujuma yoyote dhidi yake inapolazimika kufanya hivyo.

Brigedia Jenerali Ahmad Reza Pourdastan ameongeza kuwa, katika hali ambayo Tehran daima imesimama dhidi ya madola ya kibeberu na ya kivamizi, sera yake kuu ni kuimarisha uhusiano na ushirikiano na nchi jirani zake.

Iran imekuwa ikisisitiza kuwa, uwezo wa kiulinzi wa Jamhuri ya Kiislamu ni kwa ajili ya kukabiliana na chokochoko zozote za adui na si kwa madhara ya nchi rafiki.

Tags