Khatibzadeh: Marekani inafungamanisha masuala ya kibinadamu na malengo ya kisiasa
https://parstoday.ir/sw/news/iran-i72534-khatibzadeh_marekani_inafungamanisha_masuala_ya_kibinadamu_na_malengo_ya_kisiasa
Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran amesema kuwa mazungumzo kuhusu kubadilishana wafungwa yamefanyika kwa nyakati tofauti huko Vienna na kusisitiza kuwa kile inachofanya Marekani ni kufungamanisha kadhia ya kibinadamu na malengo ya kisiasa.
(last modified 2023-11-27T08:44:11+00:00 )
Jul 19, 2021 06:38 UTC
  • Khatibzadeh: Marekani inafungamanisha masuala ya kibinadamu na malengo ya kisiasa

Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran amesema kuwa mazungumzo kuhusu kubadilishana wafungwa yamefanyika kwa nyakati tofauti huko Vienna na kusisitiza kuwa kile inachofanya Marekani ni kufungamanisha kadhia ya kibinadamu na malengo ya kisiasa.

Akizungumza leo asubuhi na waandishi wa habari hapa Tehran, Saeed Khatibzadeh ameeleza kuwa, suala la kuhuisha mapatano ya JCPOA limechelewa kutokana na hatua na misimamo ya Marekani ambayo imedai kuwa sasa tunapasa kusubiri kuanza kazi serikali mpya ya Iran. Amesema ni wazi kuwa siasa jumla za mfumo hazibadiliki na serikali ndio mtekelezaji wa maagizo ya mfumo. Ni kawaida mazungumzo hayo yaendelee katika mkondo wa kawaida. 

Mapatano ya JCPOA yaliyopasishwa na Baraza la Usalama la UN 

Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran amebainisha kuwa, Iran itarejea kutekeleza ahadi na majukumu yake kwa mujibu wa mapatano ya JCPOA na baada ya kujiridhisha kuwa serikali ya Marekani nayo imeanza kutekeleza majukumu yake kwa mujibu wa azimio nambari 2231 la Baraza la Usalama.  

Kuhusu uamuzi wa Mahakama ya Ulaya kuhusu hijab, Khatibzadeh ameeleza kuwa: Uamuzi uliochukuliwa na chombo hicho cha sheria cha Ulaya unafedhehesha.  Amesema, pale haki za binadamu, haki za walio wachache na haki za kidini zinapoigusa na kuufikia Uislamu na Waislamu huwa na maana ndogo huko Ulaya. Uamuzi huo ni wa kibaguzi na unaochochea vitendo vya kibaguzi na unaweza kuzidisha vitendo vya chuki dhidi ya Uislamu na machafuko dhidi ya Waislamu kuendelea barani Ulaya. 

Katika kikao chake na waandishi wa habari, Msemaji wa Chombo cha Diplomasia cha Iran ameashiria pia hali ya sasa katika mipaka ya Iran na Afghanistan na kueleza kuwa: Iran inadhibiti na kufuatilia kwa makini hali ya usalama katika mipaka yake. Usalama wa Afghanistan ni usalama wetu na hatuwezi kuvumilia machafuko yanayojiri nchini humo, amesema Saeed Khatibzadeh.