SEPAH: Tunaiunga mkono harakati yoyote inayopambana na Uzayuni duniani
Kamanda wa Kikosi cha Quds cha Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu SEPAH amesema kuwa, tunaiunga mkono harakati yoyote inayopambana na utawala wa Kizayuni duniani na uungaji mkono huo utaendelea.
Katika kipindi siku 20 zilizopita, kumetokea operesheni kadhaa za kujitolea kufa shahidi zilizofanywa na vijana wa Kipalestina huko Tel Aviv na katika maeneo mengine ya ardhi za Palestina zilizopachikwa jina bandia la Israel. Operesheni hizo ni uthibitisho wa kufikia mwisho subira ya Wapalestina mbele ya jinai wanazofanyiwa kila leo na Wazayuni.
Kwa mujibu wa shirika la habari la IRNA, Brigedia Jenerali Esmail Qaani, Kamanda wa Kikosi cha Quds cha Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu SEPAH amesema hayo leo Alkhamisi katika kumbukumbu ya mwaka wa kwanza tangu kuuawa shahidi Hijazi, aliyekuwa Kaimu wa Kamanda wa Kikosi cha Quds cha Jeshi la SEPAH na kuongeza kuwa, vijana wa Palestina hivi sasa wanaendesha operesheni za kishujaa ndani ya ardhi zao zinazokaliwa kwa mabavu na Wazayuni.
Vijana hao ni rasilimali kubwa kwa taifa la Palestina na kwamba kizazi cha nne na tano cha wanamapambano wa Palestina kinafanya operesheni za kishujaa kama hizo ambazo zimevuruga mifumo yote ya kiulinzi ya utawala wa Kizayuni wa Israel.
Amesisitiza kuwa, Iran itaendelea kupambana vilivyo na mabeberu wakiwemo Wazayuni ambao amesema, dola hilo pandikizi ni dhaifu mno kuweza kusimama kukabiliana na nguvu za Jamhuri ya Kiislamu ya Iran. Ameongeza kuwa, kwa jinai zake za kila leo, utawala wa Kizayuni unazidi kuharakisha kuangamizwa kwake kikamilifu.