Kikao cha nchi za Kiarabu na Kiislamu cha Riyadh chatoa taarifa rasmi ya maamuzi muhimu kadhaa
Kikao cha wakuu wa nchi za Kiarabu na Kiislamu kilichofanyika mjini Riyadh, Saudi Arabia kimetilia mkazo ulazima wa kuondolewa mzingiro dhidi ya Gaza na kuingia misafara ya misaada ya kibinadamu katika eneo hilo.
Sehemu moja ya taarifa hiyo imesema: "tunalitaka Baraza la Usalama lichukue uamuzi wa haraka kulaani uharibifu wa kinyama uliofanywa na Israel katika hospitali za Ukanda wa Gaza. Aidha tunazitaka nchi zote ziache kuwapelekea silaha na zana za kivita viongozi wa utawala ghasibu."
Taarifa ya mwisho ya kikao cha wakuu wa nchi za Kiarabu na Kiislamu imesisitiza pia kwamba hata vikihalalishwa kwa kisingizio chochote kile, inapinga maelezo ya kuviita vita vya ulipizaji kisasi dhidi ya Gaza kuwa ni hatua ya kujilinda.
Washiriki wa mkutano wa wakuu wa nchi za Kiarabu na Kiislamu wamesisitiza pia katika taarifa ya mwisho ya mkutano wao kwa kusema: "tunalaani hatua ya kutaka kuwahamisha Wapalestina wapatao milioni moja na nusu kutoka kaskazini mwa Ukanda wa Gaza na kuwapeleka kusini, ambayo inachukuliwa kuwa uhalifu wa kivita kulingana na Mkataba wa Nne wa Geneva wa 1949 na kiambatisho chake cha mwaka 1977. Na tunazitaka pande zinazohusika na makubaliano ya Geneva zichukue maamuzi na hatua za pamoja katika kuulaani hatua hiyo, na pia tunazitaka taasisi zote zinazohusika za Umoja wa Mataifa kukabiliana na njama za viongozi wa utawala ghasibu za kuendeleza hali hii ya kusikitisha na isiyo ya kibinadamu na kutilia mkazo haja ya kurejea haraka wakimbizi wa Kipalestina kwenye makazi na maeneo yao".
Taarifa hiyo imeeleza bayana kuwa kuwahamisha kwa nguvu, kuwabaidisha au kuwalazimisha Wapalestina waondoke kwenye maeneo yao iwe ni ndani ya Ukanda wa Gaza au Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan ikiwa ni pamoja na Baitul Muqaddas, au nje ya eneo hilo na kuwapeleka mahali pengine popote ni mstari mwekundu na ni uhalifu wa kivita.../