Klabu Bingwa Ulaya: Arsenal yainyuka 2-0 Basel, Walcott ang'ara
Michuano ya klabu bingwa barani Ulaya imeendelea katika hatua ya makundi ambapo usiku wa kuamkia leo viwanja vinane vilikuwa msambweni wakati klabu za makundi mbalimbali zilipokutana kuwania pointi tatu muhimu.
Wabeba Bunduki wa London Arsenal ya Uingereza wakiwa nyumbani walibuka na ushindi wa mabao 2 kwa nunge dhidi ya Basel ya ya Uswisi huku magoli yote yakiwekwa kimiani na winga machachari Theo Walcott.
PSG ya Ufaransa ikiwa ugenini iliibuka na ushindi mnono wa 3-1 dhidi ya Ludogorets Razgrad ya nchini Bulgaria.
Besiktas imeenda sare ya 1-1 dhidi ya Dynamo Kyiv. Huku SSC Napoli ikiibuka na ushindi wa 4-2 dhidi ya Benfica.
Borussia Moenchengladbach nayo ikiwa nyumbi imekubali kichapo cha 2-1 kutoka kwa Barcelona ya Uhispania. Na mchezo wa kushangaza wa funga nikufunge ulikuwa kati ya Celtic na Manchester City, ambapo timu hizo zilienda sare ya kufungana mabao 3-3.
Atletico Madrid nayo ikiwa nyumbani ilifanya kazi kubwa baada ya kuibuka na ushindi wa 1-0 dhidi ya Bayern Munich. Vijana hao wa Madrid wangeweza kupata ushindi mnono lakini walikosa penalty. Na FC Rostov ikiwa nyumbani ililazimishwa sare ya 2-2 na timu ya PSV Eindhoven.