Ronaldo; Saudi Arabia na mashabiki wa Iran
https://parstoday.ir/sw/news/west_asia-i102456-ronaldo_saudi_arabia_na_mashabiki_wa_iran
Cristiano Ronaldo, nyota wa soka wa Ureno anayechezea klabu ya An-Nasr ya Saudia Arabia, ambaye alisafiri kuja hapa Tehran kwa ajili ya pambano na timu ya Persepolis ya Iran la mashindano ya Ligi ya Mabingwa ya Asia, amepata makaribisho makubwa ya mashabiki wake.
(last modified 2026-05-06T11:35:21+00:00 )
Sep 20, 2023 05:36 UTC
  • Ronaldo; Saudi Arabia na mashabiki wa Iran

Cristiano Ronaldo, nyota wa soka wa Ureno anayechezea klabu ya An-Nasr ya Saudia Arabia, ambaye alisafiri kuja hapa Tehran kwa ajili ya pambano na timu ya Persepolis ya Iran la mashindano ya Ligi ya Mabingwa ya Asia, amepata makaribisho makubwa ya mashabiki wake.

Vyombo mbalimbali vya habari katika eneo hili na kwengineko duniani vimeakisi na kuonyesha picha za mapokezi makubwa aliyopata Ronaldo mjini Tehran; na kila chombo kimetoa uchambuzi wake juu ya kadhia hiyo. Baadhi ya vyombo vimezitumia picha hizo kuchafua sura ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran na watu wa Iran, baadhi ya vingine vimeipongeza Saudi Arabia kwa kumleta nyota huyo mkubwa wa kandanda kwenye soka la Asia, na baadhi ya vyombo vimetetea vitendo vya mashabiki wa Kiirani kwa Ronaldo.
Kulia: Mashabiki wakisindikiza basi lililombeba Ronaldo. Kushoto: Ronaldo

Ukweli ni kwamba, kupata Ronaldo mapokezi makubwa ya Wairani halikuwa tukio lisilotarajiwa au halijawahi kutokea mfano wake. Lilikuwa tukio la kawaida, ambalo kwa kuzingatia hadhi ya watu mashuhuri, wakiwemo wa michezo, na hasa aliyeshinda mara tano zawadi ya mpira wa dhahabu duniani, Ballon d'Or, lingeweza kutokea katika nchi nyingine yoyote ambayo huenda ikawa ni nadra kwa watu kuweza kuwaona kwa karibu watu mashuhuri kama hao. Wakati nyota wa soka wa Argentina Lionel Messi alipojiunga na klabu ya Paris Saint-Germain ya Ufaransa, au wakati timu ya taifa ya soka ya  Argentina ilipotembelea China hivi karibuni ikiwa pamoja na Messi, nyota huyo wa kandanda alipata mapokezi makubwa ya mashabiki wake. Sababu ya msingi zaidi ya kupata mapokezi makubwa watu kama hao, ni ukweli kwamba wao wanachukuliwa kama nembo na mfano kwa kizazi cha sasa katika nchi zote duniani ikiwemo Iran.

Ronaldo katika picha ya pamoja Tehran na mtoto mpenzi wa soka

Suala jengine ni kwamba mapokezi makubwa aliyopata Cristiano Ronaldo ni fursa na nukta chanya kwa soka la Iran na kwa soka la Saudia pia. Ronaldo, soka la Saudia na vyombo vya habari vimeelewa hadhi na nafasi ya soka nchini Iran na rasilimali ya kijamii ya michezo iliyopo Iran. Klabu ya Al-Nasr ya Saudi Arabia, ambayo ilifurahishwa sana na mapokezi iliyopewa na Wairani, ilitumia misamiati ya kuvutia katika ujumbe ilioweka kwenye mtandao wake wa X, ambapo sambamba na kuambatisha picha za watu waliokuwa wakilisindikiza basi lililombeba Ronaldo, imewashukuru watu wa Iran na kuandika: "Hiki ndicho kitu kisichoweza kununulika! " Klabu hiyo ya soka ya Saudi Arabia imeandika hivyo kuashiria mtaji wa rasilimaliwatu wa soka ulioko nchini Iran.

Mapokezi makubwa aliyopta Ronaldo mjini Tehran yalikuwa fursa na neema kwa Saudi Arabia pia. Kitendo hicho cha mashabiki wa soka wa Iran waliojawa na shauku kimeonyesha kuwa, licha ya kutumia gharama kubwa kwa kuwekeza katika soka, vilabu vya mpira wa miguu vya Saudia vimeijaza shauku na msisimko mkubwa jamii ya wapenzi wa soka wa Saudia na Ligi ya Mabingwa wa Asia.

Somo kubwa linalopatikana katika mapokezi ya aina yake aliyopata Ronaldo mjini Tehran inapasa lielekezwe kwa Shirikisho la Soka la Asia, AFC. Mchezo wa kandanda unasisimua na kuvutia kwa kuwa na watazamaji. Kwa kuinyima timu ya Persepolis fursa ya kuwa na watazamaji wake katika mechi ya jana na Al-Nasr ya Saudi Arabia, AFC imelikosesha soka la Asia fursa maalumu ya upendeleo. Shirikisho la Soka la Asia lingeweza kuiadhibu Persepolis kwa namna nyingine lakini likaruhusu watazamaji laki moja kuhudhuria kwenye Uwanja wa Azadi na kuifakharisha hadhi ya soka barani Asia kwa FIFA, nchi za Ulaya na hata Amerika.  AFC ingeliweza jana kutoa mshtukizo maalumu kwa Ronaldo na kwa watazamaji wa Iran, lakini imeinyima Persepolis, AFC yenyewe, Ronaldo na Al-Nasr ya Saudia Arabia fursa ya kunufaika na mtaji wa rasilimaliwatu wa Iran. Katika muktadha huo, Saad al-Harthi, mwanahabari maarufu wa soka wa Saudia, ameandika kwenye ukurasa wa X: "Shirikisho la Soka la Asia limefanya kosa kubwa kwa kuwanyima mashabiki wa Persepolis fursa ya kuhudhuria mechi ya timu yao dhidi ya Al-Nasr".../