Feb 25, 2018 15:36 UTC
  • Saudia yahujumu na kuvunja misikiti katika mashambulio yake mapya nchini Yemen

Ndege za kivita za utawala wa Aal-Saud zimelenga misikiti na vituo vingine vya Kiislamu katika hujuma zake mpya za anga nchini Yemen.

Kwa mujibu wa tovuti ya habari ya Yemen ya Sahafah24, shambulio la ndege hizo za Saudi Arabia limeulenga msikiti mmoja katika mji wa Ma’rib wilayani Sirwah leo Jumapili na kuuharibu kikamilifu.

Hapo jana ndege hizo za muungano wa kijeshi unaoongozwa na utawala wa Riyadh zililenga msikiti mwingine na vituo kadhaa vya kidini katika mji wa Sa’ada wilayani Razih. Aidha watu wawili walijeruhiwa katika shambulio jingine la anga la Saudia katika mji wa Sa'ada wilayani Sahar hapo jana.

Kanali ya televisheni ya al-Masirah imerusha mkanda wa video unaoonyesha namna ndege hizo za kijeshi za Aal-Saud zilivyoshambulia barabara katika mkoa wa Saqayn na kuisambaratisha kwa makusudi, mbali na kumjeruhi mwanamke mmoja. 

Moja ya misikiti iliyohujumiwa na Saudia nchini Yemen

Saudi Arabia ambayo inaungwa mkono kikamilifu na Marekani na baadhi ya nchi za Kiarabu katika eneo mwezi Machi mwaka 2015 ilianzisha uvamizi wa kijeshi dhidi ya Yemen na kisha kuiweka nchi hiyo chini ya mzingiro wa nchi kavu, baharini na angani.

Makumi ya maelfu ya wananchi wa Yemen wameuawa hadi sasa na mamilioni ya wengine kuwa wakimbizi tangu Saudia iivamie kijeshi nchi hiyo masikini ya Kiarabu. Miundombinu ya Yemen pia imeharibiwa pakubwa kufuatia uvamizi wa kijeshi wa Saudi Arabia. 

Tags