Amnesty International yaitaka Saudi Arabia iwaachie huru wafungwa wa Kipalestina
Shirika la Msamaha Duniani la Amnesty International limeutaka utawala wa Saudi Arabia uwaachilie huru wafungwa wawili wa Kipalestina ikisisitiza kwamba, kesi ya Wapalestina hao haikuendeshwa kiadilifu.
Katika ujumbe wake kwa Mfalme Salman bin Abdul Aziz wa Saudi Arabia, Shirika la Msamaha Duniani la Amnesty International limesema kuwa, Muhammad al-Khidhr na mwanawe Hani al-Khidhr wanapaswa kuachiliwa huru kwani kesi yao haikuendeshwa kwa mujibu wa vigezo vya kimataifa na kwamba, kesi yao haikufanyika kiadilifu.
Shirika hilo la kutetea haki za binadamu limeeleza kwamba, tuhumu wanazokabiliwa nazo wafungwa hao wa Kipalestina hazina msingi wowote.
Hivi karibuni, Ismail Hania, Mkuu wa Ofisi ya Kisiasa ya Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Palestina HAMAS amesisitiza juu ya ulazima wa kuachiliwa huru haraka iwezekanavyo wafungwa wa Kipalestina wanaoshikiliwa nchini Saudi Arabia.
Ismail Hania alisisitiza kuwa, kuachiliwa huru wafungwa wa Kipalestina wanaoshikiliwa nchini Saudi Arabia imekuwa ni dharura ya kibinadamu na kitaifa, hasa baada ya kuibuka virusi vya Corona ambavyo vinatishia uhai wa wafungwa hao.
Zaidi ya Wapalestina 60 wanashikiliwa katika magereza ya Saudi Arabia wakituhumiwa kuwa na uhusiana na Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Palestina HAMAS.
Baadhi ya duru zinasema kuwa, raia wa Palestina waliokamatwa nchini Saudi Arabia na wanaoendelea kushikiliwa katika magereza ya nchi hiyo wamekuwa wakifanyiwa mateso mbalimbali.