Kinara wa Al Qaeda asema wanaisaidia Saudia vitani Yemen
Kinara mmoja wa kundi la kigaidi la Al Qaeda amekiri kuwa kundi hilo linashirikiana kwa karibu na muungano vamizi wa Saudi Arabia katika vita dhidi ya Yemen.
Khalid Saeed Batarfi, kinara wa Al Qaeda katika Bara Arabu (AQAP) amenukuliwa na Televisheni ya Al Mayadeen akisema magaidi wa kundi hilo wanapigana bega kwa bega na wanajeshi wa muungano vamizi wa Saudi Arabia wanaoshirikiana na wanamgambo watiifu kwa rais wa zamani wa Yemen Abd Rabbuh Mansur Hadi dhidi ya Jeshi la Kitaifa la Yemen na Harakati ya Ansarullah.
"Nafasi yetu katika kupigana dhidi ya Mahouthi (Ansarullah) iko wazi na hakuna anayeweza kukana hilo," amesema Batarfi.
Aidha amebaini kuwa, magaidi hao wa Al Qaeda wamekuwa wakishirikiana na wanajeshi wa Saudia na mamluki wao katika medani 11 za kivita dhidi ya Jeshi la Kitaifa la Yemen na Ansarullah.
Mapema mwaka huu, Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani wa Yemen Meja Jenerali Abdul Majid Al-Murtadha alisema katika taarifa kuwa walifanikiwa kunasa idadi kubwa ya zana za kivita zilizokuwa zikitumiwa na al Qaeda katika mkoa wa Al Bayda na kwamba ushahidi ulionyesha kuwa magaidi hao wanapata msaada kutoka mashirika ya kijasusi ya kigeni.

Mwezi Machi 2015, Saudi Arabia ilianzisha mashambulizi makubwa ya kivamizi dhidi ya wananchi wa Yemen kwa uungaji mkono kamili wa Marekani, utawala wa Kizayuni wa Israel, madola mengine ya kibeberu ya Marekani na kwa ushirikiano mkubwa na Umoja wa Falme za Kiarabu (Imarati) na baadhi ya nchi za Kiarabu kama Sudan pamoja na makundi kadhaa ya kigaidi kama vile Al Qaeda.
Tangu wakati huo hadi sasa madola hayo vamizi yameizingira kila upande Yemen kutokea angani, baharini na ardhini na hawaruhusu chochote kuingia wala kutoka nchini humo. Hiyo ni jinai nyingine kubwa inayofanywa na wavamizi wa nchi ya Kiislamu ya Yemen.
Hadi sasa uvamizi huo wa Saudia na kundi lake umeshasababisha makumi ya maelfu ya Wayemen kuuawa, wengine wengi kujeruhiwa huku mamilioni ya wengine wakiwa wakimbizi ndani na nje ya nchi.