Mar 22, 2024 02:26 UTC
  • Msomi Myahudi akosoa vikali UN kushindwa kuchukua hatua juu ya Ghaza kutokana na kura za veto

Mtengenezaji filamu mashuhuri wa Kiyahudi Haim Bresheeth, ambaye pia ni mpiga picha na msomi mtajika amekosoa vikali Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kushindwa kuchukua hatua katika mzozo wa utawala wa Kizayuni wa Israel na Palestina kutokana na kura ya turufu inayoshikiliwa na wanachama wake watano wa kudumu.

Akielezea wasiwasi wake juu ya kushindwa Baraza la Usalama kuchukua hatua madhubuti katika kukabiliana na mashambulio na mauaji ya kinyama yanayoendelea kufanywa na Israel huko Ghaza, Bresheeth amesema: "Umoja wa Mataifa haupaswi kuwa na Baraza la Usalama lenye wajumbe watano ambao wanaweza kupiga kura ya turufu. Nadhani hiyo iko wazi kabisa, sio tu kwamba si kidemokrasia, lakini si mantiki kwamba ulimwengu mzima unapiga kura za kufanya jambo, kisha nchi moja inapiga kura ya turufu. Huu ni wendawazimu".
 
Msomi huyo ameashiria dharau inayoonyeshwa na utawala wa Kizayuni kwa sheria za kimataifa na akasema: "Hawaheshimu sheria za kimataifa hata kidogo. Wanajua kwamba wanatetewa na Magharibi yote, na Magharibi yote inaunga mkono mauaji ya kimbari na uhalifu wa kivita unaofanywa na Israel".
 
Profesa Bresheeth amezungumzia pia jinsi wanachama watatu wa kudumu wa Baraza la Usalama (Marekani, Uingereza na Ufaransa) zinavyoona raha kupigia kura ya veto azimio lolote linalotaka kupitishwa dhidi ya Israel, na kuitaja hali hiyo ni kuporomoka kwa kanuni za kimataifa zilizowekwa na Wamagharibi wenyewe.
Mabalozi wa US na UK wakipinga azimio la usitishaji vita Ghaza katika Baraza la Usalama la UN

Ameeleza pia kwamba amekamilisha filamu aliyotengeneza kuhusu hali ya Ghaza, hata hivyo amesema ana shaka kama itaweza kuonyeshwa nchini Uingereza kutokana na muelekeo wake wa kupinga Uzayuni.

Profesa Bresheeth amevikosoa pia vyombo vya habari vya Magharibi kwa kupuuza mateso ya Wapalestina na kuakisi zaidi uungaji mkono wa Magharibi kwa Israel licha ya kushutumiwa kwa mauaji ya kimbari.

Halikadhalika, msomi huyo amezungumzia kutimuliwa wasomi na utawala wa Kizayuni wa Israel kwa kuzungumza dhidi ya mauaji ya kimbari yanayofanywa na utawala huo huko Ghaza na akasema, muelekeo sawa na huo unafuatwa nchini Uingereza, ambako vyuo vikuu vimewafukuza maprofesa kadhaa na kuchukua hatua dhidi ya wanafunzi pia.

“Nina maprofesa kadhaa ninaowajua waliofukuzwa kazi Israel kwa sababu wamesema kinachoendelea Ghaza si ubinadamu na hakipasi kuungwa mkono kwa vyovyote vile. Nchini Uingereza, vyuo vikuu vimewafukuza kazi maprofesa kadhaa na kuchukua hatua dhidi ya wanafunzi, wengi wao wakiwa ni Wapalestina na Wayahudi, ambao wameandamana kupinga vita, wakitaka kusitishwa mapigano".../

Tags