Unicef yakosoa kutoheshimu sheria pande zinazozozana Libya
Mjumbe Maalumu wa Mfuko wa Kuhudumia Watoto wa Umoja wa Mataifa (Unicef) nchini Libya amezitaka pande zinazozozana nchini humo kuheshimu sheria za kimataifa.
Abdulrahman Ghandour amesema kuwa ripoti zilizotolewa hadi sasa zinazoonyesha idadi ya watoto walioaga dunia kufuatia mlipuko wa kigaidi uliotekelezwa juzi katika eneo la al Salman katika mji wa Benghazi mashariki mwa Libya, ni za kutisha. Mjumbe maalumu wa Unicef huko Libya amesema kitendo cha kuwalenga watoto na mashambulizi ya kigaidi hakikubaliki kivyovyote vile na kuzitolea wito pande zote husika katika mzozo huko Libya kuwajibika mbele ya jamii ya kimataifa.
Watu wasiopungua 34 waliuawa na wengine 87 wakiwemo watoto kadhaa walijeruhiwa baada ya magari mawili yaliyotegwa bomu kulipuka juzi Jumanne mbele ya msikiti mmoja na karibu na idara inayoshughulikia hati za kusafiria katika mji wa Benghazi mashariki mwa Libya.