Askari watano wa Marekani wauawa, saba wajeruhiwa nchini Afghanistan
Msemaji wa kundi la Taliban, Dhabihullah Mujahid amesema kundi hilo limewaangamiza askari watano wa Marekani nchini Afghanistan.
Katika taarifa aliyotoa mapema leo, msemaji huyo wa Taliban amesema, katika mapigano yaliyotokea mkoani Qunduz kaskazini mwa Afghanistan kati ya wanajeshi wa Marekani wakishirikiana na vikosi vya serikali ya Afghanistan na kundi la Taliban, askari watano wa Marekani wameuliwa na wengine saba wamejeruhiwa.
Katika taarifa yake hiyo, Dhabihullah Mujahid ameongeza kuwa, askari 18 wa jeshi la Afghanistan pia wameuawa na wengine 13 wamejeruhiwa katika mapigano hayo.
Kamandi ya uongozi wa majeshi ya Marekani na wa shirika la kijeshi la NATO imetoa taarifa ya kuthibitisha kuuawa askari wawili wa Marekani nchini Afghanistan lakini haikutoa ufafanuzi kuhusu kuuawa kwao.
Tangu Marekani ilipopeleka majeshi yake nchini Afghanistan mwaka 2001 hadi sasa, zaidi ya askari wake 2,400 wameuliwa na wengine wasiopungua 20,200 wamejeruhiwa.
Na hii ni pamoja na kuwa, wananchi wa Afghanistan wanapinga majeshi ya kigeni yakiongozwa na Marekani kuweko nchini mwao, na kutaka Washington ihitimishe uwepo wake kijeshi katika ardhi ya nchi hiyo.../