Pakistan: Wamarekani sio watu wa kuaminika
Waziri wa Reli nchini Pakistan amesema kuwa, Wamarekani sio watu wa kuaminika kwa namna yoyote ile kwa kuwa huko nyuma pia waliihadaa Pakistan.
Sheikh Rasheed Ahmad ameyasema hayo kwenye kikao na waandishi wa habari mjini Islamabad ambapo ameashiria ahadi kadhaa za uongo za Marekani kwa nchi yake. Ahmad ameongeza kuwa, uongo wa Marekani kwa Pakistan uliisukuma Islamabad upande wa baadhi ya nchi za eneo ikiwemo China. Aidha Waziri wa Reli wa Pakistan amezungumzia hatua ya kuyafutia mamlaka maalumu maeneo ya Jammu na Kashmir iliyotekelezwa na serikali ya India na kusema kuwa kitendo hicho ni ukiukaji wa sheria za kimataifa na kuongeza kwamba, Islamabad ipo tayari kuwapigania wakazi wa Kashmir haki zao.
Ameonyesha matumaini kuwa, suala la Kashmir litatatuliwa kwa njia ya mazungumzo. Waziri wa Reli wa Pakistan ametoa matamshi ya kutokuwa na imani na Wamarekani katika hali ambayo Imran Khan, Waziri Mkuu wa nchi hiyo amefanya safari nchini Marekani ambapo pia anatazamiwa kukutana na Rais Donald Trump wa nchi hiyo.