Uturuki na Russia zatupilia mbali sarafu ya dola katika biashara
(last modified Thu, 10 Oct 2019 04:19:50 GMT )
Oct 10, 2019 04:19 UTC
  • Uturuki na Russia zatupilia mbali sarafu ya dola katika biashara

Uturuki na Russia zimetia saini mapatano ya kutupilia mbali sarafu ya dola katika mabadilishano ya kibiashara baina yao.

Wizara ya Fedha ya Russia imetangaza kuwa, kwa mujibu wa mapatano yaliyotiwa saini, sarafu za Ruble ya Russia na Lira ya Uturuki zitatumika katika malipo na miamala ya kifedha baina ya nchi mbili.

Kwa mujibu wa mapatano hayo, nchi hizo mbili zitaanza kutekeleza hatua kwa hatua mpango huo wa kutumia sarafu za kitaifa katika biashara ya pande mbili. Biashara baina ya nchi hizo iliongezeka kwa silimia 16 mwaka jana na kufika dola bilioni 25.5.

Aidha mapatano hayo yanalenga kuunganisha banki za Uturuki na mfumo wa kimataifa wa mabadilishano ya kifedha wa Russia ambao umechukua sehemu ya ule wa kimataifa wa SWIFT unaosimamiwa na Marekani.

Kadi ya MIR ya Russia inatazamiwa kuchukua nafasi ya kadi za VISA na MasterCard za Marekani duniani

Aidha banki za Uturuki zitawezeshwa kutumia mfumo wa kadi za benki za MIR za Russia ambazo zinachukua nafasi ya zile kadi za benki za Kimarekani za VISA na MasterCard. Mapatano hayo ni katika mkakati wa nchi hizo mbili kuacha kutegemea sarafu ya dola ya Marekani.

Hivi karibuni Gavana wa Banki Kuu ya Iran Abdolnaser Hemmati alitangaza kuwa  Uturuki,  Iran na Russia zimeafikiana kuacha kutumia sarafu ya Marekani na badala yake kutumia za ndani katika biashara kati ya mataifa  hayo matatu.