Umoja wa Mataifa wakosoa ukandamizaji unaofanywa dhidi ya waandamanaji nchini Marekani
Maandamano makubwa na yasiyo na mfano wake ambayo yamekuwa yakifanyika nchini Marekani tokea kuuawa kinyama kwa Mmarekani mweusi George Floyd katika mji wa Minnesota katika jimbo la Minneapolis tarehe 25 Mei, yangali yanaendelea licha ya ukandamizaji mkubwa unaofanywa na serikali ya Trump dhidi ya waandamanaji.
Ofisi ya Haki za Binadamu ya Umoja wa Mataifa siku ya Ijumaa ilikosoa vikali serikali ya Trump kwa kuwakandamiza waandamanaji ambao wanalalamikia ubaguzi wa rangi nchini humo na kusisitiza kwamba askari usalama na polisi ya nchi hiyo haipasi kukandamiza wala kuwatia nguvuni kinyume cha sheria, waandamanaji na waandishi habari wanaoakisi maandamano hayo. Ofisi hiyo ya kimataifa imesema kuwa maafisa wanaovunja sheria wanapaswa kutambuliwa na kisha kufikishwa mbele ya vyombo vya sheria ili kujibu mashtaka kuhusu ukiukaji huo. Baadhi ya miji muhimu ya Marekani ikiwa ni pamoja na Portland katika jimbo la Oregon, siku hizi imekuwa kitovu cha maandamano ya kulalamikia ubaguzi wa rangi, yaliyoanza tokea kuuwa kwa George Floyd.
Akizungumza hivi karibuni na waandishi habari huko Geneva, Liz Throssell, Msemaji wa Ofisi ya Haki za Binadamu ya Umoja wa Mataifa ameseme: 'Ni muhimu sana kwa watu kup

ewa fursa ya kulalamika kwa njia ya amani na wala hawapaswi kukabiliwa na vitendo visivyofaa na vya kibaguzi.' Amebainisha wasi wasi mkubwa alionao kuhusiana na ripoti zinazosema kuwa waandamanaji wamekuwa wakitiwa nguvuni na watu wasiojulikana waliovalia nguo za raia na kupelekwa kusikojulikana na kusema, huenda kitendo hicho kilicho kinyume cha sheria kikahalalishwa rasmi nchini humo.
Hii si mara ya kwanza kwa Umoja wa Mataifa kulalamikia ukandamizaji unaofanywa dhidi ya waandamanaji wanaopinga ubaguzi wa rangi na uonevu huko Marekani. Michelle Bachelet, Kamishna Mkuu wa wa Haki za Binadamu wa Umoja wa Mataifa mwanzoni mwa mwezi Juni mwaka huu alilalamikia vikali ubaguzi wa kimfumo nchini Marekani na kushambuliwa waandishi wa habari ambao wamekuwa wakiakisi maandamano makubwa yanayofanywa na Wamarekani kuhusu suala hilo. Alisema katika taarifa: Sauti za watu wanaotaka kukomeshwa mauaji dhidi ya Wamarekani weusi hazina silaha na hivyo zinapaswa kusikilizwa. Vilevile sauti zinazotaka kukomeshwa ukandamizaji wa polisi na ubaguzi wa kimfumo ulioenea pakubwa katika jamii ya Marekani zinapaswa kusikilizwa.
Kwa kutangaza mpango wa kutumwa askari wa serikali kuu ya Marekani katika majimbo ya nchi hiyo yanayodaiwa kuwa yamekumbwa na machafuko ya wahuni, Trump anakusudia kutumia mkono wa chuma kuwakandamiza waandamanaji wanaoshiriki katika maandamano ya kisheria dhidi ya ubaguzi wa rangi na uoneu katika nchi hiyo. Amesema kuwa yuko tayari kutuma askari 60,000 katika miji tofauti ya nchi hiyo ili kukabiliana na wale anaowatuhumu kuwa ni wahuni na waibuaji ghasia na machafuko. Licha ya vitisho hivyo vya Trump ambaye anatambuliwa na wengi kuwa mbaguzi mkubwa wa rangi, si tu kwamba mandamano hayajapungua bali yamepata kasi zaidi katika pembe tofauti za nchi hiyo.

Ukweli ni kwamba maandamano hayo yamepata kasi na msukumo mpya kutokana na kuwa serikali ya Trump ambayo inaunga mkono ubaguzi wa rangi na utumiaji mabavu wa kimfumo, imekuwa ikiwaruhusu polisi kuitumia nguvu za ziada dhidi ya weusi wa nchi hiyo. Ukweli huo umewapelekea wajuzi wengi wa mambo kuamini kwamba machafuko na vitendo vya mabavu vimeongezeka zaidi nchini Marekani katika kipindi hiki cha utawala wa rais huyo mbaguzi.
Takwimu zilizotolewa na Polisi ya Federali ya Marekani FBI zinathibitisha wazi kwamba tokea aingie madarakani Trump, vitendo vya mauaji ya kutisha na utumiaji mabavu dhidi ya weusi vimeongezeka sana nchini humo. Kwa msingi huo ni wazi kuwa msimamo wa kibaguzi wa Trump na uungaji mkono wake wa dhahiri na wa siri kwa vitendo vya wabaguzi wa rangi, umekuwa na nafasi kubwa katika kudumisha na kuimarisha ukandamizaji dhidi ya raia weusi wa nchi hiyo katika miaka ya hivi karibuni. Muamala wa kibaguzi wa Trump dhidi ya waandamanaji wanaopinga dhuma na ubaguzi nchini Marekani, yaani nchi inayojinadi kuwa mtetezi mkuu wa demokrasia na uhuru duniani, unathibitisha wazi uongo wa madai hayo yanayokusudiwa kuuhadaa ulimwengu.