Uchunguzi: Familia milioni 26 nchini Marekani zinakabiliwa na njaa
Matokeo ya uchunguzi mpya uliofanywa nchini Marekani yanaonyesha kuwa, familia milioni 26 nchini humo hazina chakula cha kutosha.
Mtandao wa Kanali ya Televisheni ya CNN umeripoti kuwa, uchunguzi huo unaonyesha kuwa, familia milioni 26 nchini Marekani haziwezi kujikimu kwa chakula kutokana na kutokuwa na uwezo na fedha za kutosha za kununua chakula.
Aidha sehemu nyingine ya uchunguzi huo inaonyesha kuwa, asilimia 20 ya watu wazima wenye watoto wadogo wamesema kuwa, katika wiki za hivi karibuni hawakuwa na fedha za kutosha kwa ajili ya kununua chakula.
Kadhalika uchunguzi huo unaonyesha kuwa, wananchi wa Marekani wenye kukabiliwa na uhaba mkubwa wa chakula wanahitajia msaada wa haraka wa ili waweze kukimu mahitaji yao kama hasa ya chakula.
Wakati huo huo, ripoti mbalimbali zinaonyesha kuwa, licha ya ahadi chungu nzima alizotoa Rais Donald Trump wa Marekani za kupunguza kiwango cha umasikini nchini humo, lakini idadi ya watu wanaotaabika kwa ufakiri na umasikini imeongezeka katika miaka ya hivi karibuni.
Inaelezwa kuwa, akthari ya Wamarekani wamekata tamaa kabisa na utendaji wa sasa na wa baadaye wa serikali ya Trump katika suala zima la uchumi na hivyo wanazieleza siasa za Trump kwamba, ndizo zilizopelekea kuongezeka umasikini nchini humo na hivyo kuyafanya maisha yao kuwa magumu siku baada ya siku.