Hillary Clinton akiri kuwa utawala wa Saudia ndio uliomuua Jamal Khashoggi
Mgombea urais aliyeshindwa katika uchaguzi wa mwaka 2016 nchini Marekani amekiri kuwa utawala wa Saudi Arabia ndio uliomuua mwandishi wa habari Jamal Khashoggi aliyekuwa mkosoaji mkubwa wa utawala huo.
Hillary Clinton, ambaye pia ni waziri wa zamani wa mambo ya nje wa Marekani, ameyasema hayo katika ujumbe aliotuma kwenye ukurasa wake wa twitter alioambatanisha na tangazo la filamu iitwayo "Mpinzani" inayosimulia maisha ya Jamal Khashoggi, hadi muda alipouawa ndani ya ubalozi mdogo wa Saudi Arabia mjini Istanbul, Uturuki; na kusisitiza kuwa utawala wa Aal Saud ndio unaobeba dhima ya mauaji ya mwandishi huyo wa habari.
Jamal Khashoggi aliuawa kinyama tarehe Pili Oktoba, 2018 kisha mwili wake ukakatwa vipandevipande.
Kwa muda wa siku 18 tangu yalipofanyika mauaji hayo ya kikatili utawala wa Saudia ulinyamaza kimya na hata kukanusha kutokea kwake, mpaka ripoti za serikali ya Uturuki na Shirika la Ujasusi la Marekani CIA zilipothibitisha kuwa mauaji ya Jamal Khashoggi yalifanywa kwa amri ya moja kwa moja iliyotolewa na Mohammad bin Salman, mrithi wa ufalme wa Saudi Arabia.../