Kamala Harris akiri kuwepo silaha nyingi Marekani
Makamu wa Rais wa Marekani amekiri kuwa, silaha zilizopo nchini humo ni nyingi zaidi ya watu wa nchi hiyo.
Kamala Harris ameeleza kuwa idadi ya silaha zilizopo nchini Marekani zimepindukia idadi ya watu wa nchi hiyo na kuwa ni tishio zaidi kwa raia wa Marekani wenye asili ya Afrika.
Bi Kamala ambaye alikuwa akihutubia Mkutano wa Taasisi ya The NAACP au National Association for the Advancement of Colored People ambayo ni taasisi kongwe na kubwa zaidi ya haki za kiraia nchini Marekani ameongeza kuwa, idadi ya silaha zilizoundwa Marekani miaka 20 iliyopita zimeongezeka mara tatu zaidi na sasa zimekuwa nyingi kupita wananchi wa nchi hiyo.

Makamu wa Rais wa Marekani aidha amesisitiza kuwa raia wa Marekani wenye asili ya Afrika ndio wahanga zaidi wa mashambulizi ya kutumia silaha nchini humo; na pamoja na kuwa raia weusi wanaunda asilimia 13 ya jamii ya nchi hiyo lakini asilimia 62 ya wahanga wa mashambulizi ya silaha nchini humo ni raia weusi.
Takwimu zinaonyesha kuwa, mashambulizi ya silaha na ufyatuaji risasi kiholela nchini Marekani mwaka mmoja uliopita yameua zaidiya watu elfu 19 na kujeruhi zaidi ya elfu 37. Aidha kuna silaha moto zaidi ya milioni 300 nchini Marekani.