Askari wa UN auawa Jamhuri ya Afrika ya Kati
Umoja wa Mataifa umetangaza kuwa askari wake mmoja wa kulinda amani ameuawa katika Jamhuri ya Afrika ya Kati.
Kikosi cha Umoja wa Mataifa cha kulinda amani katika Jamhuri ya Afrika ya Kati MINUSCA kimetangaza kuwa, watu waliokuwa na silaha wamemuua askari mwingine wa umoja huo katika mji wa Bangui.
MINUSCA imetangaza kuwa askari huyo ni raia wa Senegal na kwamba imeanza uchunguzi kuhusu mauaji hayo ambayo imesema hayakubaliki.
Mwakilishi wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa katika Jamhuri ya Afrika ya Kati pia amesema kuwa mashambulizi dhidi ya askari wa kulinda amani ni jinai ya kivita.
Askari wa kulinda amani wa Umoja wa Mataifa wamekuwa wakishambuliwa na kuuawa katika maeneo mengi wanakolinda amani barani Afrika.
Askari wa Umoja wa Mataifa walitumwa katika Jamhuri ya Afrika ya Kati mwaka 2014 kwa shabaha ya kulinda amani katika nchi hiyo iliyokuwa katika machafuko na vita vya wenyewe kwa wenyewe.