Waziri Mkuu wa Niger: Balozi wa Ufaransa hana nafasi katika nchi yetu
https://parstoday.ir/sw/news/africa-i101878-waziri_mkuu_wa_niger_balozi_wa_ufaransa_hana_nafasi_katika_nchi_yetu
Waziri Mkuu wa Niger amemtaka balozi wa Ufaransa kuondoka mara moja nchini humo.
(last modified 2023-11-27T12:14:11+00:00 )
Sep 05, 2023 07:36 UTC
  • Ali Muhammad al-Amin Zain
    Ali Muhammad al-Amin Zain

Waziri Mkuu wa Niger amemtaka balozi wa Ufaransa kuondoka mara moja nchini humo.

Ali Muhammad al-Amin Zain, waziri mkuu aliyeteuliwa na baraza la kijeshi la Niger, amesema katika mkutano na waandishi wa habari jana Jumatatu kwamba: "Uwepo wa vikosi vya jeshi la Ufaransa nchini Niger ni kinyume cha sheria, na balozi wa Ufaransa hana nafasi katika nchi yetu."

Ali Muhammad al-Amin Zain pia amesisitiza kuwa vikwazo dhidi ya Niger si halali, na kuongeza kuwa zinafanyika jitihada kubwa za kushinda vikwazo vilivyowekwa na nchi nyingi dhidi ya Niger.

Waziri Mkuu wa Niger amebainisha zaidi kwamba: Uchunguzi wote kuhusu utawala wa "Mohammed Bazoum" utawasilishwa katika mahakama zinazofaa na kwamba serikali ya sasa haitaingilia taratibu hizo.

al-Amin Zain amesema kwamba Niamey inatarajia "kufikia makubaliano ndani ya siku chache" na Jumuiya ya Kiuchumi ya Afrika Magharibi (ECOWAS), ambayo imetishia kuingilia kijeshi na kumrejesha madarakani Rais Mohamed Bazoum.
"Hatukuacha mawasiliano na ECOWAS, tunaendelea na mawasiliano," amesema Ali Muhammad al-Amin Zain.

Jumatano, 26 Julai 26, vikosi vya gadi ya rais wa Niger vilimkamata rais wa nchi hiyo, Mohammed Bazoum, ndani ya ikulu ya rais kwa tuhuma za ufisadi, kula njama na nchi za Magharibi, na kupuuza umaskini, na kisha kumuondoa madarakani.

Katika siku za hivi karibuni, watu wa Niger, wamekuwa wakifanya maandamano na kutangaza uungaji mkono wao kwa baraza la kijeshi la nchi hiyo. Vilevile wanataka kuondolewa kwa wanajeshi wa Ufaransa nchini Niger.