Vikosi vya usalama vyawekwa katika hali ya tahadhari nchini Misri
Askari wa vikosi vya usalama wamesambazwa katika miji mbalimbali ya Misri, na vyombo vya usalama vimetangaza kuweko hali ya tahadhari nchini kote.
Askari usalama wametawanywa katika vituo na maeneo muhimu ya mji mkuu wa Misri, Cairo zikiwemo barabara zinazoishia kwenye uwanja wa Tahrir kwa lengo la kuzuia maandamano yaliyoitishwa kufanyika hii leo.
Hapo awali, watumiaji wa mitandao ya kijamii walikuwa wametoa wito kupitia kurasa zao za kijamii wa kuwataka wananchi wa Misri washiriki kwenye maandamano yaliyopangwa kufanyika katika miji yote ya nchi hiyo leo Ijumaa kulalamikia hali mbaya ya kiuchumi na kijamii inayotawala nchini humo.
Mitandao ya kijamii imeyataja maandamano hayo kuwa ni 'Mapinduzi ya Mafakiri'.
Ripoti zinaeleza kuwa vyama kadhaa na mirengo mbalimbali yenye satua ya kisiasa nchini Misri imetangaza kuunga mkono maandamano hayo.
Yasir al-Amdah, mratibu mkuu na msemaji wa Harakati ya Mafakiri nchini Misri amesema harakati hiyo haiwakilishi walalahoi na wenye njaa pekee bali ni mwakilishi wa Wamisri wote wanaodhulumiwa.
Mbali na hali mbaya ya usalama, Misri inakabiliwa pia na matataizo ya kiuchumi, ufisadi wa mali za umma, kupungua kiwango cha utoaji huduma za kijamii na uendeshaji usioridhisha katika nyanja zote.
Hii ni katika hali ambayo kutatua matatizo ya kiuchumi ni miongoni mwa ahadi kuu zilizotolewa na Rais Abdel Fattah el Sisi wakati wa kampeni zake za kuwania urais.../