Uchaguzi wa Bunge nchini Gabon waakhirishwa
Uchaguzi wa Bunge nchini Gabon uliokuwa umepangwa kufanyika mwezi huu wa Desemba umeakhirishwa kutokana na kutokuweko bajeti ya kutosha ya kuendesha zoezi la uchaguzi huo.
Waziri wa Mambo ya Ndani wa Gabon alitangaza jana Jumamosi kwamba, uchaguzi wa Bunge uliokuwa umepangwa kufanyika mwezi huu umeakhirishwa kutokana na kutokuweko fedha za kutosha za kuendeshea zoezi la uchaguzi huo. Mahakama ya Katiba ya Gabon imetangaza kuwa, sasa uchaguzi huo utafanyika baada ya miezi saba.
Imeelezwa kuwa, kupungua uzalishaji wa mafuta na wakati huo huo kuporomoka kwa bei ya mafuta katika soko la dunia kumeifanya Gabon ikabiliwe na nakisi ya bajeti.
Aidha mgogoro ulioibuka nchini Gabon baada ya uchaguzi wa Rais uliotawaliwa na malalamiko mengi yaliyofuatiwa na machafuko umeisababishia matatizo mengi nchi hiyo ya Kiafrika.
Kwa mujibu wa matokeo ya mwisho ya uchaguzi wa Rais yaliyotangazwa na tume hiyo ya uchaguzi, Rais Ali Bongo alimshinda mpinzani wake Jean Ping kwa kupata asilimia 49.85 ya kura dhidi ya Ping aliyepata asilimia 48.23 ya kura hizo na hivyo kupata fursa ya kuiongoza nchi hiyo kwa kipindi cha miaka mingine 7. Ping alipinga matokeo hayo mara tu baada ya kutangazwa rasmi na Tume ya Uchaguzi ya Gabon.
Katika Bunge la sasa, chama tawala cha Rais Ali Bongo kina viti 114 kati ya viti vyote 120 vya bunge hilo.