Watu 9 wauawa katika mripuko wa kigaidi, kaskazini mashariki mwa Misri
Mripuko wa bomu uliotokea kwenye eneo la al Arish katika mkoa wa Sinai Kaskazini nchini Misri, umeuawa na kujeruhi watu wasiopungua tisa.
Mtandao wa habari wa Bawwabat al Fajr wa Misri umetangaza habari hiyo na kuongeza kwamba magaidi wametegesha gari lililojaa mabomu katika njia wliyokuwa wanapita wanajeshi wa Misri kwenye eneo la al Masaid huko Sinai Kaskazini na kuliripua leo Jumatatu.
Jana pia watu wenye silaha walivamia kituo kimoja ya upekuzi katika Rasi ya Sinai, kaskazini mwa Misri na kuua wanajeshi wanne na kujeruhi wengine wanne.
Mashambulizi ya kigaidi katika mkoa wa Sinai Kaskazini na maeneo mengine ya Misri yameongezeka tangu wanajeshi wa nchi hiyo wakiongozwa na Jeneral Abdul Fattah el Sisi walipompindua Muhammad Morsi, Rais wa kwanza wa Misri kuchaguliwa na wananchi katika uchaguzi huru.
Hivi sasa magenge kadhaa yenye misimamo mikali yanafanya mashambulizi ya mara kwa mara katika mkoa wa Sinai Kaskazini ulioko kaskazini mashariki mwa Misri na kundi maarufu zaidi ni lile la Wilaya ya Sinai lililotangaza utiifu wake kwa genge la kigaidi la Daesh (ISIS).