Waasi wenye silaha wauawa na jeshi la Misri
Watu kadhaa wenye silaha wameuawa na jeshi la Misri katika mkoa wa Sinai kaskazini mwa nchio hiyo.
Wizara ya Mambo ya Ndani ya Misri imetangaza leo kwamba, jumla ya watu 10 wameuawa katika mapigano makali yaliyojiri baina ya jeshi la nchi hiyo na kundi hilo katika mkoa huo.
Katika upande mwingine vyombo vya usalama nchini Misri vimetangaza habari ya kunaswa harakati za wanachama wa kundi la amaah Ansar Baitul Maqdis katika mkoa wa Sinai chini ya uongozi wa Ahmad Mahmoud Yusuf Abdul-Qadir.
Ripoti zinasema, baada ya Abdul-Qadir kuunda kundi hilo linalojiita amaah Ansar Baitul Maqdis alianzisha mashambulizi dhidi ya askari polisi na jeshi la Misri.
Miongoni mwa operesheni zilizotekelezwa na wanachama wa kundi hilo lenye mafungamano na genge la Daesh ni kushambulia eneo la al-Matwafi na al-Masaid mjini El-Arish, hujuma zilizopelekea kuuawa polisi wanane.
Kadhalika vyombo vya usalama nchini Misri vimegundua kuwa, wanachama wa kundi hilo wanatumia maeneo ya wazi kama ngome zao ili kusalimika na operesheni za jeshi la serikali. Hadi sasa jeshi la nchi hiyo limefanikiwa kudhibiti maficho kadhaa ya kundi hilo na kunasa aina tofauti ya silaha.