UN yataka kukomeshwa haraka machafuko nchini CAR
https://parstoday.ir/sw/news/africa-i27334-un_yataka_kukomeshwa_haraka_machafuko_nchini_car
Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa limetaka kukomeshwa haraka iwezekanavyo, mapigano na vitendo vya utumiaji mabavu vya makundi ya wabeba silaha, Jamhuri ya Afrika ya Kati.
(last modified 2026-01-14T08:12:18+00:00 )
Apr 05, 2017 09:41 UTC
  • UN yataka kukomeshwa haraka machafuko nchini CAR

Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa limetaka kukomeshwa haraka iwezekanavyo, mapigano na vitendo vya utumiaji mabavu vya makundi ya wabeba silaha, Jamhuri ya Afrika ya Kati.

Taarifa iliyotolewa na baraza hilo la usalama la Umoja wa Mataifa mbali na kuonyesha wasiwasi wake juu ya mapigano hayo nchini CAR, imeyataka makundi ya wabeba silaha hususan 'Harakati ya Kitaifa kwa Ajili ya kufufua nchi FPRC' na kundi la 'Umoja kwa ajili ya Amani ya Afrika ya Kati UPC' kukomesha uhasama na mapigano yao nchini humo.

Waasi wa Seleka

Kadhali Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, limeunga mkono juhudi zinazofanywa na Rais Faustin-Archange Touadéra wa nchi hiyo za kurejesha usalama sambamba na kufufua mchakato wa mazungumzo ya amani baina ya makundi ya wabeba silaha ndani ya nchi hiyo ya katikati mwa Afrika. Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa pia limetaka kuchukuliwe hatua kali za kisheria, dhidi ya wahusika wa ukiukaji wa haki za binaadamu na vitendo vilivyo kinyume na maadili.

Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa

Mapigano ya hivi karibuni katika miji ya Bambari, Ouaka, mkoa wa katikati na Makoum, kusini mwa Jamhuri ya Afrika ya Kati, yamesababisha mauaji makubwa na wakazi wengi wa maeneo hayo kuwa wakimbizi.

Jamhuri ya Afrika ya Kati ilitumbukia katika mgogoro, mwaka 2013 baada ya kuzuka mapigano ya kikaumu yaliyopelekea kuondolewa madarakani serikali ya rais François Bozizé.