Burundi yalalamikia ripoti ya hivi karibuni ya Baraza la Haki za Binadamu
Wananchi wa Burundi wameilalamikia ripoti ya hivi karibuni ya Umoja wa Mataifa kuhusu ukiukwaji wa haki za binadamu unaofanywa na askari usalama wa nchi hiyo.
Wanaharakati wa taasisi za kiraia za Burundi zenye mfungamano na kundi linalojumuisha jumuiya za ustawi wa nchi hiyo (CODI-Burundi) wameandamana katika mji mkuu wa nchi hiyo Bujumbura kulalamikia ripoti iliyotolewa hivi karibuni na Baraza la Haki za Binadamu la Umoja wa Mataifa kuhusu ukiukaji wa haki za binadamu unaofanywa na askari usalama nchini humo.
Venuste Muyabanga Mwakilishi wa Masuala ya Sheria wa Taasisi ya Kiraia ya Burundi amesema kuwa ripoti iliyotolewa na wajumbe wa Umoja wa Mataifa kuhusu kukiukwa haki za binadamu na kuwepo machafuko huko Burundi haina itibari bila ya kutolewa maoni ya raia wa nchi hiyo.
Siku kadhaa zilizopita serikali ya Burundi ilitangaza kusimamisha shughuli za ofisi ya haki za binadamu ya Umoja wa Mataifa kufuatia kutolewa ripoti hiyo. Kabla ya hapo pia Burundi ilikuwa imezuia kuingia nchini humo wakaguzi wa haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa kutokana na kuhusika kwao katika kutengeneza filamu inayoonyesha uhalisia wa mamia ya vitendo vya unyongaji, utiaji mbaroni watu kiholela, mateso na udhalilishaji wa kijinsia unaofanywa huko Burundi.