Idadi ya walioaga dunia kwa kimbunga nchini Madagascar wafikia 51
Idadi ya watu walioaga dunia kutokana na kimbunga kilichoiathiri Madagascar siku kumi zilizopita wameongezeka na kufikia 51, huku watu wengine 22 wakiwa hawajulikani walipo hadi sasa.
Kimbunga hicho cha kitropiki kwa jina la Ava kiliikumba Madagascar kati ya tarehe 5 hadi 6 mwezi huu wa Januari na kuathiri zaidi pwani ya mashariki mwa kisiwa hicho kilichoko katika bahari ya Hindi huku upepo ukivuma kwa mwendo wa kilomita 140 hadi 190 kwa saa. Idara ya kukabiliana na maafa ya kimaumbile ya Madagascar wiki iliyopita ilitangaza kuwa watu 29 wameaga dunia kutokana na kimbunga hicho.
Idara hiyo pia jana ilitangaza katika taarifa yake kuwa watu zaidi ya 54,000 wamesalia bila ya makazi. Mwezi Machi mwaka jana kimbunga kwa jina la Enawo kiliua watu wasiopungua 78 katika pwani ya kaskazi mashariki mwa Madagascar eneo linalozalisha vanila nchini humo.