Sudan yalalamikia ripoti ya mahakama ya ICC dhidi ya nchi hiyo
Wizara ya Mambo ya Nje wa Sudan imeituhumu Mahakama ya Kimataifa ya Jinai ICC kuwa inafanya ubaguzi dhidi ya Khartoum.
Wizara ya Mambo ya Nje ya Sudan imetoa tamko maalumu na kusema kuwa, Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kama ilivyofanya huko nyuma, limesikiliza tu ripoti ya Mwendesha Mashtaka Mkuu wa Mahakama ya Kimataifa ya Jinai ICC na matamko ya nchi wanachama wa baraza hilo pamoja na taarifa iliyotolewa na Sudan na halikutoa azimio au hati au hata taarifa tu kwa vyombo vya habari.
Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Sudan amesema, taarifa za nchi nyingine wanachama wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa zinaonesha namna heshima na itibari ya mahakama ya ICC ilivyozidi kuporomoka.
Ameongeza kuwa, vitendo vya kibaguzi vinavyofanywa na mahakama hiyo vimeipotezea heshima kimataifa mahakama ya ICC na kuuweka chini ya alama ya kuuliza msingi wa kujiepusha mahakama hiyo na ushawishwi wowote wa kisiasa wa baadhi ya nchi kwake.
Itakumbukwa kuwa katika ripoti yake kwa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, Fatou Bensouda, Mwendesha Mashtaka Mkuu wa Mahakama ya Kimataifa ya Jinai ICC alisema siku ya Alkhamisi kuwa baraza hilo linapaswa kuchukua hatua madhubuti zaidi za kuhakikisha Rais Omar al Bashir wa Sudan anatiwa mbaroni na kufikishwa mbele ya mahakama hiyo kujibu mashtaka ya uhalifu wa kivita na jinai dhidi ya binadamu huko Darfur, magharibi mwa Sudan.