Watoto 10 wapoteza maisha katika mlipuko Omdurman, Sudan
Watoto wasipungua 10 wamepoteza maisha baada ya chombo kisichojulikana kulipuka katika mji wa Omdurman karibu na mji mkuu wa Sudan, Khartoum.
Taarifa zinasema watoto saba walikufa papohapo na wengine walipoteza maisha wakati akipata matibabu hospitalini.
Taarifa zinasema watoto hao walikuwa wakitafuta vyuma vilivyochakaa wakati walipokumbana na chuma "kisicho cha kawaida" ambacho kililipuka baada ya wao kukishika.
Taarifa zinasema mlipuko huo umejiri Omdurman kaskazini katika eneo ambalo liliwahi kuwa kituo cha kijeshi miaka kadhaa iliyopita.

Polisi wanasema wanachunguza tukio hilo. Idadi kubwa ya watoto nchini Sudan sasa wanalazimika ufanya kazi kuwasiadia wazazi wao kutokana na matatizo ya kiuchumi katika nchi hiyo huku bei za bidhaa za vyakula zikizidi kuongezeka.
Hali ngumu ya maisha, hasa ughali wa chakula, imepelekea kuibuke maandamano ya kitaifa ambapo wananchi wenye hasira wanataka Rais Omar al Bashir aondoke madarakani. Rais Bashir ameanzisha kampeni ya kukandamiza maandamano hayo kwa kuweka sheria ya hatari kitaifa ambayo ilianza kutekelezwa Februari 22 kuzima maandamano hayo.