Sep 10, 2019 14:37 UTC
  • Watu kadhaa wauawa katika maombolezo ya siku ya Ashura nchini Nigeria

Waislamu kadhaa waliokuwa katika maombolezo ya Siku ya Ashura (tarehe 10 Muharram) wakikumbuka mauaji ya mjukuu wa Mtume Muhammad (saw) wameuawa leo kwa kupigwa risasi nchini Nigeria.

Taarifa iliyotolewa na Harakati ya Kiislamu ya Nigeria (IMN) imesema kuwa, askari wa serikali ya Nigeria wamewafyatulia risasi Waislamu walioshiriki katika shughuli ya maombolezo ya Ashura na kuua watu wasiopungua watatu na kujeruhi makumi ya wengine. Hujuma hiyo ya askari wa jeshi la Nigeria imelenga msafara wa Waislamu walioshiriki katika shughuli ya kukumbuka mauaji ya mjukuu wa Mtume Muhammad (saw), Imam Hussein bin Ali bin Abi Twalib (as) aliyeuawa kikatili na utawala wa Bani Umayyah mwaka 61 Hijria. 

Baadhi ya Waislamu wa Nigeria wakimkumbuka Hussein bin Ali (as)

Hii si mara ya kwanza kwa askari wa Nigeria kushambulia umati wa Waislamu waliokuwa wakishiriki katika shughuli ya maombolezo na kukumbuka mauaji ya Imam Hussein (as). Mwaka jana pia jeshi la Nigeria lilishambulia mjumuiko mkubwa wa Waislamu walioshiriki maombolezo ya siku ya Ashura katika mji wa Zaria huko kaskazini mwa Nigeria na kuua shahidi watu kadhaa. 

Itakumbukwa kuwa mwaka 2015, jeshi la Nigeria lilifanya uvamizi na hujuma ya kinyama ya kuwaua na kuwajeruhi waumini wapatao elfu mbili waliokuwa kwenye hafla ya maombolezo ya Imam Hussein AS, akiwemo kiongozi wa harakati ya Kiislamu ya nchi hiyo Sheikh Ibrahim Zakzaky. Baada ya kumjeruhi vibaya kiongozi huyo, walimchukua yeye pamoja na mkewe na kumpeleka mahali kusikojulikana.

Tags