20 wauawa katika shambulizi dhidi ya mgodi wa dhahabu Burkina Faso
Kwa akali watu 20 wameuawa baada ya watu waliobeba silaha kushambulia mgodi wa dhahabu kaskazini mwa Burkina Faso.
Duru za habari zinaarifu kuwa, watu wasiojulikana ambao walikuwa wamejizatiti kwa silaha wamevamia mgodi huo katika kijiji cha Madudaji katika mkoa wa Sam kaskazini mwa nchi na kutekeleza ukatili huo.
Vyombo vya usalama katika eneo hilo vimeripoti kuwa, watu wengine kadhaa wamejeruhiwa katika hujuma hiyo ya kuvizia.
Wiki iliyopita, watu 20 waliuawa katika mashambulizi mawili tofauti ya watu waliokuwa juu ya pikipiki katika mikoa ya Bam na Sam kaskazini mwa Burkina Faso.
Serikali ya Burkina Faso kuanzia mwanzoni mwa mwaka huu hadi sasa imetangaza hali ya hatari katika majimbo saba kati ya 13 ya nchi hiyo.
Mamia ya watu wameuawa katika mashambulizi ya makundi ya kigaidi na magenge ya waasi wanaobebe silaha nchini Burkina Faso tangu mwaka 2015 hadi sasa.