Wananchi wa Tunisia waandamana kulaani mapatano ya Imarati na utawala wa Kizayuni
Wananchi wa Tunisia wamefanya maandamano makubwa kupinga mapatano yaliyofikiwa kati ya Imarati na utawala wa Kizayuni wa Israel ya kuanzisha uhusiano wa kidiplomasia kati ya pande mbili hizo.
Wananchi wa Tunisia waliandamana jana katika miji mbalimbali ya nchi hiyo wakiwa wamebebe mabango yaliyokuwa na maneno yasemayo" "Ni jinai kuanzisha uhusiano na utawala haramu."
Washiriki katika maandamano hao pia wametangaza mshikamano wao na wananchi wa Palestina na kusisitiza kwamba, lengo la mapatano hayo ni kuwapotosha walimwengu kuhusu kadhia ya Palestina.
Umoja wa Falme za Kiarabu (Imarati) na Israel tarehe 13 mwezi huu wa Agosti zilifikia mapatano ya kuanzisha uhusiano kamili wa kidiplomasia kutokana na jitihada zilizofanywa na Rais Donald Trump wa Marekani. Hata hivyo mapatano hayo yamekosolewa pakubwa katika Ulimwengu wa Kiislamu.
Fauz Barhum Msemaji wa Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Palestina (Hamas) Alhamisi iliyopita aliyataja mapatano hayo kuwa ni sawa na "malipo ya bure" ambayo Umoja wa Falme za Kiarabu umeipatia Israel kutokana na jinai unazoendelea kufanya dhidi ya Wapalestina.

Wizara ya Mambo ya Nje ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran pia imelaani kuanzishwa uhusiano wa kidiplomasia kati ya Imarati na utawala wa Kizayuni wa Israel na kueleza kuwa: Wananchi madhlumu wa Palestina na mataifa yote yanayopigania ukombozi duniani hayawezi kusamehe hata kidogo hatua hiyo ya kuanzisha uhusiano na utawala ghasibu.
Katika miezi ya karibuni, tawala za nchi za Kiarabu zimekuwa zikifaya kila ziwezalo kuanzisha uhusiano wa kidiplomasia na Israel; katika hali ambayo ni kwa miaka mingi sasa utawala huo ghasibu unayakalia kwa mabavu maeneo ya Kiarabu na Kiislamu mbali na kuwakandamiza raia wa Palestina.