Mar 12, 2024 03:13 UTC
  • Raisi: Wajibu wa wakuu wa nchi za Kiislamu ni kudumisha amani miongoni mwa Waislamu

Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amewapongeza viongozi na wananchi wa nchi za Kiislamu kwa mnasaba wa kuwadia mwezi mtukufu wa Ramadhani na kusema kuwa, ni wajibu wa viongozi wa nchi za Kiislamu kuhimiza na kudumisha amani na undugu baina ya Waislamu.

Sayyid Ebrahim Raisi, Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ameyasema hayo katika salamu zake za kheri ya kuwadia mwezi wa Ramadhani kwa viongozi na wananchi wa nchi za Waislamu na kuongeza kuwa: Palestina, Baitul Muqaddas na Msikiti wa Al-Aqsa vitarejeshwa katika Ulimwengu wa Kiislamu kwa kuendeleza mapambano ya Waislamu wa Palestina na uungaji mkono wa dhati wa Ulimwengu wa Kiislamu.

Sayyid Ebrahim Raisi

Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesisitiza kuwa, kuimarishwa uhusiano wa kindugu baina ya Umma wa Kiislamu na kupanua uhusiano kati ya nchi za Waislamu kutaimarisha na kunyanyua juu zaidi Uislamu duniani. Ameongeza kuwa: Uratibu wa nchi za Kiislamu kwa ajili ya kupambana na dhulma na unyonyaji wa mabeberu hususan utawala ghasibu wa Israel, ambao mbali na kukalia kwa mabavu ardhi tukufu ya Palestina kwa zaidi ya miongo 7 na kufanya ukatili usio na kifani katika miezi michache iliyopita, vilevile umeua shahidi zaidi ya Wapalestina elfu 31, hasa watoto wasio na hatia, utazidisha heshima na fahari ya Waislamu, hususan taifa linalodhulumiwa na kukandamizwa la Palestina, katika nyanja zote.

Mwezi wa Ramadhani umeanza leo nchini Iran na katika baadhi ya nchi za Waislamu kama Malaysia, Indonesia, Brunei, Oman, Pakistan na Iraq. 

Tags