Iran na Oman kuandaa itifaki ya Lango Bahari la Hormuz
https://parstoday.ir/sw/news/iran-i137752-iran_na_oman_kuandaa_itifaki_ya_lango_bahari_la_hormuz
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran amesema kuwa Iran na Oman zinashirikiana kuandaa itifaki ya pamoja ili kuhakikisha usafiri salama wa majini katika Lango Bahari la Hormuz katika kipindi cha baada ya vita.
(last modified 2026-04-03T03:38:43+00:00 )
Apr 03, 2026 03:38 UTC
  • Kazem Gharibabadi
    Kazem Gharibabadi

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran amesema kuwa Iran na Oman zinashirikiana kuandaa itifaki ya pamoja ili kuhakikisha usafiri salama wa majini katika Lango Bahari la Hormuz katika kipindi cha baada ya vita.

Katika mahojiano na Sputnik, Kazem Gharibabadi amesema kuwa hapo awali Lango Bahari la Hormuz lilikuwa wazi na usafiri wa majini ulikuwa ukiendelea kwa kawaida. Hata hivyo, mashambulizi ya kijeshi ya hivi karibuni na vitendo vya uchokozi vya Marekani na Israel vimevuruga upitaji salama na kusababisha changamoto kubwa.

Amebainisha kuwa kwa sasa Iran iko katika hali ya vita, na kwamba si jambo la uhalisia kutarajia sheria za wakati wa amani zitumike katika mazingira kama hayo. Aidha amesema Lango Bahari la Hormuz haliko wazi kwa tawala mbili vamizi za  Marekani na Israel pamoja na waungaji mkono wao.

Gharibabadi ameongeza kuwa hali ya sasa katika Lango Bahari la Hormuz ni matokeo ya moja kwa moja ya vitendo hivyo vya uchokozi.

Ameonya kwamba hata baada ya vita kumalizika, eneo hilo linaweza kukabiliwa na vitendo vingine vya uchokozi, akibainisha kuwa baadhi ya nchi bado zinategemea vita kama chombo cha sera. Katika hali kama hizo, alisema, vyombo vya majini vinavyomilikiwa na wavamizi na waungaji mkono wao, iwe vya kibiashara au vya kijeshi, havitaruhusiwa kupita katika mlango huo.

Amesisitiza kuwa mtazamo huo utakuwa sehemu ya sera ya kimsingi ya Iran katika hali zozote za mizozo ya baadaye. Wakati huohuo, amesisitiza kuwa katika kipindi cha amani, Iran na Oman kama nchi mbili za pwani zina dhamira ya kuhakikisha usafiri wa majini ulio salama na wenye usalama kupitia uratibu wa pamoja.

Gharibabadi amesema kuwa katika hali za kawaida, vyombo vyote vya majini vinavyopita katika Mlango wa Hormuz vitatarajiwa kufanya uratibu mapema na mamlaka za Iran na Oman na kupata vibali vinavyohitajika ili kuhakikisha usalama. Ameongeza kuwa masuala ya mazingira pamoja na usalama wa majini pia ni mambo muhimu katika mfumo huo.

Amefafanua kuwa Iran na Oman zitachukua jukumu kubwa zaidi katika kuhakikisha upitaji salama na kwa sasa zinafanya kazi ya kuandaa rasimu ya itifaki ya kudhibiti usafiri wa majini katika mlango huo wakati wa amani. Amesema itifaki hiyo haikusudiwi kuwa kizuizi, bali ni utaratibu wa kuwezesha upitaji salama na kutoa huduma bora zaidi kwa vyombo vya majini.

Gharibabadi amebainisha kuwa mchakato wa kuandaa rasimu hiyo uko katika hatua za mwisho, na kwamba baada ya kukamilika ndani ya Iran, Tehran itaanza mazungumzo rasmi na Oman ili kukamilisha itifaki ya pamoja itakayosimamia usafiri wa majini katika njia hiyo muhimu ya kimkakati.