Zarif na Sheikh Ahmad wasisitiza kuhitimishwa maafa ya kibinadamu Yemen
Waziri wa wa Mambo ya Nje wa Iran na Mjumbe Maalumu wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa katika Masuala ya Yemen wamesisitiza ulazima wa kuhitimishwa maafa ya kibinadamu huko Yemen na kupatikana njia za kisiasa ili kutatua mgogoro wa nchi hiyo.
Ismail Ould Sheikh Ahmad ambaye jana Jumamosi alifanya safari hapa Tehran kwa ajili ya mashauriano na viongozi wa Iran amekutana na kufanya mazungumzo na Muhammad Javad Zarif Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran kuhusu matukio ya hivi karibuni huko Yemen.
Sheikh Ahmad alifanya mazungumzo pia na Hussein Jaberi Ansari, Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran Anayehusika na Masuala ya Nchi za Kiarabu na Afrika ambapo pande hizo zimejadili njia za kufufua mazungumzo ya kisiasa na kutuma misaada ya kibinadamu kwa raia wa Yemen walioathiriwa na ukosefu wa chakula na mzingiro wa pande zote wa Saudi Arabia na washirika wake.
Mjumbe Maalumu wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa katika Masuala ya Yemen pia amesisitiza kwamba, mgogoro wa nchi hiyo hauwezi kutatuliwa kwa njia za kijeshi na amepongeza hatua ya Iran ya kuunga mkono ufumbuzi wa amani wa mgogoro wa Yemen na kurejeshwa amani nchini humo.