Netanyahu na uafriti wake usio na kikomo wa kukwamisha mapatano katika mazungumzo ya kusimamisha vita
(last modified Thu, 05 Sep 2024 07:30:57 GMT )
Sep 05, 2024 07:30 UTC
  • Netanyahu na uafriti wake usio na kikomo wa kukwamisha mapatano katika mazungumzo ya kusimamisha vita

Benjamin Netanyahu, Waziri Mkuu wa utawala haramu wa Kizayuni wa Israel anaendelea kukwamisha mapatano katika mazungumzo ya kusitisha mapigano katika Ukanda wa Ghaza.

Juhudi mpya za mazungumzo ya kuhitimisha vita vya Ghaza zimekuwa zikiendelea kufanywa na nchi tatu za Misri, Qatar na Marekani kwa muda wa takribani siku 20 sasa. Kila baada ya muda, hutangazwa habari za kupatikana mafanikio katika mazungumzo hayo na kukaribia kufikiwa mwafaka wa kusitisha mapigano, lakini ukweli wa habari hizo bado haujathibiti kivitendo na mauaji ya kimbari yangali yanaendelea huko Ghaza.
Netanyahu (kulia) na Blinken, waziri wa mambo ya nje wa Marekani

Netanyahu na baadhi ya mawaziri wake ndio kizuizi kikubwa zaidi kinachokwamisha kufikiwa mwafaka katika mazungumzo ya kusitisha mapigano, kwa sababu kila inapotangazwa habari ya kutia matumaini kuhusiana na mazungumzo hayo, huzua uafriti mpya wa ukwamishaji. Katika uafriti wake wa karibuni zaidi, siku ya Jumatatu Netanyahu alidai kuwa harakati ya Hamas inapata silaha kupitia Misri na Ukanda wa Philadelphia.

Matamshi hayo ya Netanyahu ni kikwazo kwa mazungumzo katika hali mbili. Kwa upande mmoja, Misri ni miongoni mwa nchi zinazofanya juhudi kubwa za kufanikisha usitishaji mapigano huko Ghaza; na kwa kushirikiana na Qatar, imekuwa mwenyeji wa vikao vya mazungumzo hayo ya kusitisha vita. Kwa upande mwingine, Philadelphia ni moja ya ajenda kuu za mazungumzo ya Doha na Cairo. Harakati ya Hamas inataka utawala wa Kizayuni uondoe kikamilifu majeshi yake katika Ukanda wa Philadelphia; na hata Marekani pia imeitaka Tel Aviv ifanye hivyo, lakini Wazayuni wanang'ang'ania msimamo wao wa kuudhibiti ukanda huo. Kwa kuzingatia hilo, na katika kujibu madai ya Netanyahu kwamba silaha zinaingizwa kimagendo Ghaza kupitia Philadelphia, Misri imetangaza kuwa madai hayo ni uafriti mwingine wa kukwamisha juhudi za kufikia makubaliano.

Wizara ya Mambo ya Nje ya Misri imetangaza katika taarifa kwamba: kwa kauli yake hiyo, na kwa kulipenyeza jina la Misri kwenye madai yake, waziri mkuu wa utawala wa Kizayuni anataka kukwamisha tena juhudi za kufikia mapatano na kuwababaisha Waisraeli kuhusiana na suala hilo. Siku ya Jumanne, Wizara ya Mambo ya Nje ya Iraq ilitoa taarifa ya kulaani madai ya waziri mkuu wa utawala wa Kizayuni kwamba silaha zinaingizwa Ghaza kutokea Misri. Taarifa hiyo ya Wizara ya Mambo ya Nje ya Iraq ilieleza bayana kuwa: Baghdad inalaani vikali matamshi ya utawala ghasibu wa Kizayuni ya kukwamisha juhudi za kusitisha vita huko Ghaza na inatangaza mshikamano na Misri dhidi ya madai hayo ya uwongo yaliyotolewa kuhusu mhimili wa Philadelphia.

Netanyahu akionyesha usanii wa kudai Philadelphia ni njia ya kupitishia silaha

Uafriti unaofanywa na Netanyahu na baraza lake la mawaziri wa kukwamisha kufikiwa mwafaka katika mazungumzo unatokana na sababu kadhaa. Sababu ya kwanza ni kwamba, hakuna makubaliano ya pamoja ndani ya baraza lake la mawaziri juu ya suala la kusitisha vita katika Ukanda wa Ghaza; na kuna baadhi ya mawaziri wenye misimamo mikali ambao wamefika hadi hata kumuonya Netanyahu kuwa watachukua hatua ya kujiuzulu katika serikali yake endapo vita vitasitishwa huko Ghaza na hivyo kuandaa mazingira ya kusambaratika serikali hiyo. Sababu ya pili ni kuwa, Netanyahu anafahamu kwamba kumalizika vita huko Ghaza kunaweza kuchochea juhudi za mrengo wa upinzani za kutamatisha maisha yake ya kisiasa, kwa sababu miezi 11 ya vita dhidi ya Ghaza haijawezesha kukombolewa mateka na kurejeshwa heshima na itibari ya taasisi za kiintelijensia na kijeshi za utawala huo. Kuhitimishwa vita vya Ghaza na kuondoka kikamilifu majeshi ya Kizayuni katika eneo hilo ni jambo linalomtia hofu na kiwewe Netanyahu kwa sababu analichukulia kama ithibati kamili ya kushindwa vibaya sana katika njama yake dhidi ya Muqawama, Ghaza na Palestina kwa ujumla.../