Jumamosi, Februari 13, 2016
Leo ni Jumamosi tarehe 4 Mfunguo Nane Jamadi al-Awwal 1437 Hijria sawa na tarehe 13 Februari mwaka 2016 Miladia.
Siku kama ya leo miaka 882 iliyopita kulingana na kalenda ya Hijria
alizaliwa huko nchini Iraq Ibn Athir Jazari mwanahistoria na mwanafasihi
mahiri wa Kiislamu. Ibn Athir alisoma mjini Mosul, Sham na Baghdad kwa
maulama watajika kama Khatib Tusi. Alikuwa na mapenzi makubwa na
kutwalii na kufanya uhakiki kuhusiana na historia na ni kutokana na
sababu hiyo athari zake nyingi zilizoko hii leo zinahusiana na historia.
Kitabu mashuhuri zaidi cha Ibn Athir ni kile kinachojulikana kwa jina
la "al-Kamil Fi Taarikh." Msomi na mwanahistoria huyo wa Kiislamu
alifariki dunia mwaka 630 Hijria katika mji wa Mosul huko Iraq. ***
Katika
siku kama ya leo miaka 327 iliyopita tangazo lililojulikana kama
Tangazo la Sheria lilisomwa katika sherehe za kumvika taji Mfalme
William wa Tatu na Malkia Marry wa Pili wa Uingereza na kuanzia hapo
mfumo wa utawala wa nchi hiyo ukabadilika na kuwa utawala wa kifalme wa
kikatiba. Kwa mujibu wa tangazo hilo, madaraka ya Mfalme wa Uingereza
yalipunguzwa na kukabidhiwa bunge la nchi hiyo. ***
Miaka 28
iliyopita katika siku kama hii ya leo, aliaga dunia Ayatullah Sheikh
Salman Khaqani. Alizaliwa mwaka 1293 Hijria Shamsia katika moja ya miji
ya kusini mwa Iraq ya leo. Baada ya kupitisha kipindi cha utoto, akiwa
na umri wa miaka 13 alihajiri na kuelekea Najaf al-Ashraf kwa ajili ya
kusoma masomo ya dini. Akiendelea na masomo yake, Sheikh Salman Khaqani
hakuacha kujihusisha na harakati za kijamii, kiasiasa na kifasihi. Akiwa
na umri wa miaka 43 na baada ya kufariki dunia baba yake aliyekuwa
mmoja wa maulama wa Khorramshahr hapa Iran aliuchagua mji huo kuwa
makazi yake. Katika kipindi cha miongo mitatu ya kuishi kwake mjini
Khorramshahr, mwanazuoni huyo aliondokea kuwa chimbuko la uongofu wa
watu na kufanikiwa kutoa huduma zenye thamani kubwa. Baada ya kuanza
vita vya miaka minane vilivyoanzishwa na utawala wa Baath wa Iraq,
nyumba ya alimu huyo ilikuwa kimbilio la watu.