Wazayuni wayafanya maisha kuwa magumu huko Jabalia, Ukanda wa Gaza
Wanajeshi wa utawala wa Kizayuni wameifanya hali ya mambo na maisha kuwa ngumu katika eneo la Jabalia kwa lengo la kuwahamisha kwa nguvu wakazi wa Kipalestina wa mji huo.
Gazeti la Kizayuni la Haaretz limefichua takwimu za kutisha zinazoonyesha hali mbaya wanayopitia raia wa Kipalestina katika eneo la Jabalia katika miezi miwili ya karibuni.
Haaretz limeandika kuwa, takwimu zinaonyesha namna wanajeshi wa Israel wanavyotumia nguvu kuwalazimisha raia wa Palestina elfu 96 kuondoka katika kambi ya Jabalia huku waliosalia wakibaki katika mazingira magumu.
Takwimu hizo zinaendelea kubainisha kuwa, karibu asilimia 70 ya nyumba katika kambi ya wakimbizi ya Jabalia zimebomolewa na kuharibiwa kikamilifu na kuna uwezekano idadi hiyo ikaongezeka kutokana na kuendelea mashambulizi na mauaji ya kimbari ya Israel.
Wanajeshi wa utawala wa Israel wameuzingira kikamilifu mji na kambi ya Jabalia kwa zaidi ya siku 75 huku wakiendeleza hujuma za nchi kavu, angani na baharini dhidi ya Gaza kiasi kwamba maeneo mengi ya ukanda huo yameharibiwa kabisa katika eneo hilo.