Radiamali ya Iran kuhusu kupigwa marufuku adhana misikitini huko Quds
Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran amezitolea wito jamii ya kimataifa na nchi za Kiislamu kufanya juhudi ili kuzuia kubadilishwa utambulisho wa Kiislamu wa Baitul Muqaddas.
Akitoa radiamali yake hapo jana kwa hatua ya baraza la mawaziri la Israel ya kupasisha mpango wa kupiga marufuku adhana katika misikiti ya Baitul Muqaddas na vile vile kuidhinisha sheria ya kuporwa ardhi za Wapalestina huko katika Ukingo wa wa Magharibi wa Mto Jordan, Bahram Qassemi amesema kuwa mpango huo unadhihirisha kuendelea kwa siasa na vitendo vilivyo dhidi ya ubinadamu, ubaguzi, vilivyo dhidi ya haki za binadamu na vya kidhulma vya utawala wa Kizayuni dhidi ya wananchi madhlumu wa Palestina kwa zaidi ya miongo sita sasa.
Bahram Qassemi ameongeza kuwa Israel inatekeleza hatua hizo lengo pekee likiwa ni kuifanya hali ya maisha ya wananchi wa Palestina kuwa mbaya zaidi katika ardhi za mababu zao na kubadili utambulisho wa Kiislamu wa Baitul Muqaddas. Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran ameitaka jamii ya kimataifa na hasa nchi za Kiislamu kutonyamaza kimya mbele ya hatua hizo za kichokozi na dhidi ya binadamu za utawala wa Kizayuni na kutotoa mwanya wa kutumbukizwa hatarini utambulisho wa Kiislamu wa Baitul Muqaddas kutokana na hatua kama hizo.